51 wakamatwa Kilimanjaro

51 wakamatwa Kilimanjaro

Muktasari:

  • Jeshi la polisi Mkoani Kilimanjaro limekamata watuhumiwa 51 wa makosa mbalimbali wakiweno 11 wa matukio ya mauaji na 40 waliokuwa wakijihusisha na uuzaji wa dawa za kulevya katika maeneo ya mkoa huo.

Moshi. Jeshi la polisi Mkoani Kilimanjaro limekamata watuhumiwa 51 wa makosa mbalimbali wakiweno 11 wa matukio ya mauaji na 40 waliokuwa wakijihusisha na uuzaji wa dawa za kulevya katika maeneo ya mkoa huo.

Akizungumza leo Septemba 20, 2021na waandishi wa habari, Kamanda wa polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Simon Maigwa, amesema watuhumiwa hao walikamatwa katika operesheni maalum ilofanyika kipindi cha Septemba 10 hadi 19, 2021.

Amesema watu hao wamekuwa wakijuhusisha na uuzwaji, usafirishaji wa dawa za kulevya pamoja na utengenezaji wa pombe haramu ya gongo.

Kamanda amesema katika operesheni hiyo jeshi hilo limekamata pombe ya gongo lita 105, misokoto ya bangi 3,075 sawa na kilo tano, mirungi kilo 241, pikipiki mbili, na gari moja aina ya Grand Mark II, ambavyo vilitumika kusafirishia dawa za kulevya aina ya bangi na mirungi.

"Kati ya watuhumiwa 40 waliokamatwa watuhumiwa 29 wamefikishwa mahakama na watuhumiwa 11 kesi zao zipo chini ya upelelezi na pindi upelelezi ukikamilika watafikishwa makamani," amesema Maigwa.

Amesema kwa upande wa usalama barabarani jeshi hilo limefanikiwa kukamata pikipiki 240 kwa makosa mbalimbali ya barabara.