Adaiwa kujipatia fedha kwa kuua ndugu zake -2

Muktasari:

  • Ni kesi yenye msisimko mkubwa Afrika Kusini. Inamhusu Nomia Rosemary Ndlovu, ambaye ni askari polisi wa zamani nchini humo. Tuhuma dhidi yake ni kuua watu sita. Wote ni ndugu zake.

Ni kesi yenye msisimko mkubwa Afrika Kusini. Inamhusu Nomia Rosemary Ndlovu, ambaye ni askari polisi wa zamani nchini humo. Tuhuma dhidi yake ni kuua watu sita. Wote ni ndugu zake.

Mwendesha mashitaka wa kesi hiyo, Riana Williams, ameshasoma mashitaka yote na kumtuhumu Rosemary kuwa aliwapa kazi wauaji, Lakhiwe Mkhize na Njabulo Kunene, kwa ajili ya kutekeleza kazi hiyo.

Ndugu waliouwa ni wafuatao; wa kwanza ni Witness Madala Homu. Huyu ni binadamu wa Rosemary. Aliuawa mwaka 2012. Halafu, mwaka 2013, ikawa zamu ya dada wa Rosemary, Audrey Samisa Ndlovu.

Mwaka 2015, aliyekuwa mpenzi wa Rosemary, Maurice Mabasa aliuawa. Maurice na Rosemary walifanikiwa kupata mtoto mmoja. Mwaka 2016, 2017 na 2018, Rosemary kwa kuwatumia Mkhize na Kunene, aliwaua watoto wawili wa ndugu zake, Zanele Motha, Mayeni Mashaba na Brilliant Mashego.

Tuingie mahakamani

Uhusika wa Rosemary mahakamani umekuwa na vitimbi vingi. Kuanzia kejeli kwa waandishi wa habari, aliowaambia kwamba wanamsaidia kumfanya awe mtu maarufu, hadi ndani ya kesi yenyewe.

Upo wakati Rosemary amekuwa akijenga uhusika wa mtu aliyechanganyikiwa na wakati mwingine akifanya mambo ndani ya mahakama mithili ya mtu asiyejua mahali alipo na nidhamu anayopaswa kuwa nayo.

Jaji anayesikiliza kesi hiyo, Ramarumo Monama, mara kadhaa amekuwa akimwonya Rosemary kwa kuonyesha vitendo visivyofaa ndani ya mahakama na kujaribu kukwepa kujibu maswali.

Septemba 27, mwaka huu, ndani ya Mahakama Kuu ya Gauteng, Johannesburg, Jaji Monama alimwonya Rosemary kuacha kufanya mzaha mahakamani na kukwepa maswali, na kumjulisha kwamba vitendo vyake atavikuta siku atakapomsomea hukumu.

“Nataka nisisitize kuwa nilitaka afanye utambuzi. Nitashughulika na hili kwenye hukumu yangu. Mahakama haipaswi kuingia kwenye majibizano yoyote na wewe. Nimeweka kauli yangu katika suala la utambuzi wa mwili wa Mashego,’’ alisema.

Itaendelea kesho