Adakwa na polisi akituhumiwa kusimamia kiwanda cha kutengeneza gongo

Kamanda wa Polisi mkoa wa Arusha, Justine Masejo akionesha vifaa mbalimbali vilivyokamatwa kwa mtuhumiwa anayesimamia kiwanda bubu cha kutengeneza pombe kali eneo la Sakina jijini Arusha leo.

Muktasari:

  • Jeshi la Polisi mkoani Arusha limemkamata mwanamke mwenye umri wa miaka 31 mkazi wa Sakina kwa tuhuma za kusimamia kiwanda bubu kinachotengeneza pombe inayodhaniwa kuwa gongo.

Arusha. Jeshi la Polisi mkoani Arusha limemkamata mwanamke mwenye umri wa miaka 31 mkazi wa Sakina kwa tuhuma za kusimamia kiwanda bubu kinachotengeneza pombe inayodhaniwa kuwa gongo.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Justine Masejo amesema leo Jumanne Mei 25, 2021 baada ya upekuzi katika kiwanda hicho wamekamata stika 340 za Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na stika za usalama pakiti tatu.

Amesema kingine walichokamata ni stika 700 za pombe,  vifungashio vya chupa boksi 23, chupa ndogo 483 za pombe kali, chupa kubwa 533 za pombe kali na mtambo mmoja wa kutengeneza pombe na pipa lililojaa pombe kali lita 250.

Amebainisha kuwa upelelezi unaendelea na ukikamilika jalada litapelekwa  ofisi ya Taifa ya  mashtaka kwa hatua zaidi za kisheria.

“Nitoe wito kwa wananchi kuendelea kutoa taarifa za uhalifu  na wahalifu ili kutokomeza kabisa uhalifu  katika mkoa wetu,  pia nitoe onyo kuwa zoezi hili litakua endelevu  na tutaendelea kuchukua hatua kali  kwa watu wenye nia ya kufifisha  ubora wa bidhaa za viwandani,” amesema Masejo