Ajuza aliyepigania ardhi miaka 20 afariki dunia

Muktasari:

  • Mwanaisha Mohamed, bibi wa miaka 110 ambaye kwa zaidi ya miaka 20 alikuwa akipigania ekari 12 za ardhi alizodai kudhulumiwa na Manispaa ya Ilala, amefariki bila kujua hatma ya mali yake hiyo.

Dar es Salaam. Mwanaisha Mohamed, bibi wa miaka 110 ambaye kwa zaidi ya miaka 20 alikuwa akipigania ekari 12 za ardhi alizodai kudhulumiwa na Manispaa ya Ilala, amefariki bila kujua hatma ya mali yake hiyo.

 Mwanaisha amefariki dunia Jumatano wiki hii asubuhi nyumbani kwake Kivule Magore, Wilaya ya Ilala, baada ya kuugua kwa wiki kadhaa, familia yake imethibitisha.

Tangu mwaka 2001, bibi huyo alikuwa akiingia katika ofisi mbali mbali za umma na vyombo ya kutoa haki, akiomba arudishiwe ardhi yake iliyopo katika kijiji cha Magore, Kata ya Kitunda, Wilaya ya Ilala, bila mafanikio.

Katika umri huo, Mwanaisha alikuwa akifika mwenyewe Mahakama Kuu (Divisheni ya Ardhi) na mkongojo wake kufuatilia hatma ya ardhi yake.

“Sijui kama nitaipata haki yangu kabla sijafa…nimechoka sana na hili gogoro (mgogoro) mwanangu, limenimaliza nguvu zote!,” alisema Bi Mwanaisha katika mohojiano na gazeti hili mwaka jana, huku akilia kwa uchungu.

Bi Mwanaisha alifungua ombi la kukata rufaa nje ya muda wa kisheria katika Mahakama Kuu (Divisheni ya Ardhi) baada ya Baraza la Ardhi na Nyumba Wilaya ya Ilala kutupilia mbali kesi yake ya kudai ardhi, likisema alishindwa kuthibitisha umiliki wa ardhi anayodai kurithi kutoka kwa baba yake.

Bibi Mwanaisha aliingia katika mgogoro na Manispaa ya Ilala mwaka 2001, baada ya uongozi wa Shule ya Msingi Magore B kudaiwa kuvuka mipaka ya eneo la shule na kuingia katika ardhi yake.

Wakati mgogoro ukiendelea, uongozi wa shule ulianza kuweka mawe ya mipaka, kitendo ambacho yeye na watoto wake walikipinga. Bi Mwanaisha alijaliwa watoto 16 na hadi mauti yanamfika alikuwa amebakisha watoto wawili tu.

Baada ya kuvutana na uongozi wa shule na kulalamika Manispaa ya Ilala kwa miaka kadhaa bila mafanikio, Mwanaisha aliamua kufungua shauri namba 238 katika Baraza la Ardhi na Nyumba Wilaya ya Ilala mwaka 2008, ikiliomba litoe amri ya kuwaondoa ‘wavamizi’ wa ardhi yake.

Kwa upande wao, menejimenti ya shule ilisisitiza kuwa eneo hilo ni lao baada ya kupewa na dada yake Halima Binti Mbegu kwa ajili ya ujenzi wa shule.

Katika baraza la ardhi, shauri la Mwanaisha lilisikilizwa kwa miaka kumi (2008-2018) kabla ya chombo hicho cha kutatua migogoro ya ardhi kulitupilia mbali, likidai kuwa kikongwe huyo alishindwa kuthibitisha kuwa alirithi eneo hilo kutoka kwa baba yake.

“Kesi inaitwa baada ya miezi mitatu au minne, tukifika tunaambiwa imeahirishwa. Wenzetu miaka yote hawaleti mashahidi. Mtoto wa kike nashinda njaa kutwa, wanangojea nife? alihoji Mwanaisha.

Katika maombi aliyofungua Mahakama Kuu, Mwanaisha anadai, kupita wakili wake Kasanda Mitungo, kulikuwa na ukiukwaji mkubwa wa taratibu za usikilizwaji na kurekodi mwenendo wa shauri lake katika baraza la ardhi.

Alidai kuthibitisha pia kuwa pembezoni mwa eneo hilo kulikuwa na makaburi ya familia yake yanayotambulika na serikali ya mtaa.