Hello

Your subscription is almost coming to an end. Don’t miss out on the great content on Nation.Africa

Ready to continue your informative journey with us?

Hello

Your premium access has ended, but the best of Nation.Africa is still within reach. Renew now to unlock exclusive stories and in-depth features.

Reclaim your full access. Click below to renew.

ATCL yasitisha safari za kwenda Afrika Kusini

Muktasari:

ATCL yatangaza rasmi kusitisha safari za JohanessburgAfrika Kusini, abiria waliokuwa wamekata tiketi za safari ya kuanzia Oktoba 7, 2019 watarudishiwa nauli zao.

Dar es Salaam. Shirika la Ndege la Tanzania (ATCL) limesitisha rasmi safari zake kati ya Dar es Salaam na Johanessburg, Afrika Kusini kuanzia Oktoba 7, 2019 na abiria mbao tayari walikuwa wamekata tiketi kuanzia siku hizo watarudishiwa nauli zao.

Taarifa iliyotolewa na ATCL Oktoba 3, 2019 na kusainiwa na Mkurugenzi Mkuu wa Shirika hilo, Ladislaus Matindi iliwaelekeza mawakala wa tiketi wote kurejesha nauli za wateja hao ambao tayari walikuwa wamekata tiketi.

“Sababu ni hiyo hiyo iliyoelezwa awali kama kungekuwa na nyingine tungeeleza na kama kutakuwa na la ziada tutaeleza hapo baadaye kama tulivyoeleza hili.”

“Lakini tunajipanga tukishakuwa vizuri tutarejea” alisema Matindi alipoulizwa jana Jumamosi Oktoba 5, 2019 endapo kuna sababu ya kusitishwa kwa safari hizo tofauti na ile ya awali.

ATCL ambayo ilikuwa ikifanya safari hiyo mara nne kwa wiki (Jumatatu, Jumatano, Ijumaa na Jumapili) iliacha kufanya safari kati ya miji hiyo Agosti 23,2019 baada ya ndege yake aina ya Airbus A220-300 kuzuiliwa katika uwanja wa Oliver Tambo jiji Johanessburg kwa amri ya mahakama kuu ya Guateng.

Baada ya takribani wiki mbili ndege hiyo iliachiwa huru kwa uamuzi wa mahakama.

Awali, ilielezwa baada ya kuachiwa kwa ndege hiyo safari zingeanza mara moja lakini siku moja baadaye Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Isack Kamwelwe alisema Serikali imeamua kusitisha safari kwenda katika nchi hiyo kutokana machafuko yaliyokuwa yakiendelea dhidi ya wahamiaji kutoka Afrika (Xenophibia).

Hata hivyo, kwa kipindi chote Mkurugenzi Mkuu wa ATCL, Ladislausi Matindi alikuwa akisema safari hizo ambazo awali alizitaja kama chanzo kikubwa cha mapato ya shirika hilo zingerejea baada ya kuweka mambo sawa.

Aidha tangu Agosti 23, 2019 ATCL imekuwa ikisafirisha abiria wake wa Johanessburg kwa kutumia ndege za mashirika mengine ikiwemo South African Airways, Kenya Airways, Rwanda Air na Mengine.