Bajeti ya Wizara ya Kilimo yapaa kwa zaidi ya asilimia 29

Waziri wa Kilimo, Hussein Bashe akiwasilisha makadirio ya mapato na matumizi ya wizara yake kwa mwaka 2023/2024 leo Mei 8, 2023 bungeni jijini Dodoma. Picha na Merciful Munuo

Muktasari:

  • Katika kuboresha sekta ya kilimo nchini, Serikali imeongeza bajeti ya Wizara ya Kilimo kwa asilimia 29.24

Dar es Salaam. Bajeti ya Wizara ya Kilimo imekuwa ikipaa kwa miaka mitatu mfululizo ambapo kwa mwaka 2022/23 imepanda kutoka Sh751.12 hadi kufikia Sh970.78 bilioni mwaka 2023/24 sawa na ongezeko la asilimia 29.24.

 Bajeti ya wizara hiyo katika mwaka 2021/22 ilikuwa ni Sh294.16 bilioni.

Waziri wa Kilimo Hussein Bashe ameyasema hayo leo Jumatatu Mei 8, 2023 wakati akiomba kuidhinishiwa fedha hizo na Bunge.

Amesema kati ya fedha hizo, Sh767.83 bilioni ni fedha za maendeleo.

Bashe amesema mwaka 2022/2023 fedha zilizoidhinishwa ni Sh751.12 bilioni ambapo fedha za maendeleo zilikuwa Sh569.97 bilioni na hivyo ongezeko hilo ni Sh197.86 bilioni ambazo ni fedha za maendeleo na siyo matumizi ya kawaida.

“Fedha hizo zimetengwa kwa ajili ya kuimarisha utafiti wa kilimo, uzalishaji wa mbegu, utoaji wa ruzuku, kilimo cha umwagiliaji, miundombinu ya uhifadhi wa mazao, kuimarisha huduma za ugani, upatikanaji wa masoko ya mazao na kuendeleza programu ya Jenga Kesho iliyo bora,”amesema.