Binti wa miaka 24 ashinda ubunge Kenya

New Content Item (1)
New Content Item (1)

Muktasari:

  • Binti wa miaka 24 Linet Toto, ametangazwa na Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) Kenya kuwa mshindi wa kiti cha ubunge wa Viti Maalumu kwenye Kaunti ya Bomet akiwashinda wagombea wengine wanane kwenye kinyang’anyiro hicho.

Nairobi. Binti wa miaka 24 Linet Toto, ametangazwa na Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) Kenya kuwa mshindi wa kiti cha ubunge wa Viti Maalumu kwenye Kaunti ya Bomet akiwashinda wagombea wengine wanane kwenye kinyang’anyiro hicho.

Toto ambaye kwa mara ya kwanza amegombea nafasi hiyo kupitia chama cha UDA ametangazwa mshindi baada ya kupata kura 242,775 na kumfanya kuwa mwanasiasa mdogo zaidi kujiunga na Bunge la 13.

Hata hivyo, Mbunge mteule huyo, ametaja ukosefu wa fedha kwenye kampeni zake kama changamoto kubwa aliyokumbana nayo.

“Sikuwa na fedha ya kufanya kampeni maana mimi nimetoka kuhitimu elimu yangu ya chuo hivi karibu na hicho ndio kilikuwa kikwazo changu kwenye uchaguzi wa mwaka huu,”amesema.

“Nilikuwa ni mdogo kati ya wagombea wote tisa ambao nilikuwa nao kwenye ushindani na pengine ni wakubwa kuliko mama yangu,”ameongeza.

Bunge la Kenya linaundwa na idadi ya weabunge 349 ambao miongoni mwao 47 ni wabunge wanawake (viti maalumu) ambao wanatoka kwenye kila kaunti nchini humo.

Kenya ilifanya Uchagu Mkuu Agosti 9, 2022 na hivi sasa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka inaendelea kuhakiki na kutangaza kura za urais.

Hata hivyo matokeo ya awali yanaonyesha mgombea wa Kenya Kwanza, William Ruto anaongoza kwa kupata kura milioni 6.7 akifutatiwa kwa karibu na  mgombea wa Azimio la Umoja, Raila Odinga mwenye kura 6.6.