Bodi ya mikopo yaongeza Sh84 bilioni kwa wanafunzi

Mkurugenzi Mtendaji wa HESLB Abdul-Razaq Badru .

Muktasari:

  • Bajeti ya mikopo ya elimu ya juu imeongezeka kiasi cha Sh84 bilioni na kufikisha Sh654 bilioni.

Dar es Salaam. Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu Tanzania (HESLB) imethibitisha ongezeko la bajeti ya mikopo kwa mwaka wa masomo 2022/2023 kwa asilimia 14.7 ikilinganishwa na kiasi kilichotengwa awali.

Mkurugenzi Mtendaji wa HESLB Abdul-Razaq Badru amesema kutokana na ongezeko hilo la fedha kwa sasa bajeti ya mikopo imefikia Sh654 bilioni kutoka Sh570 bilioni iliyotengwa hapo awali.

Kiasi hicho kitawezesha wanafunzi 28,000 kupata mikopo kwa robo ya kwanza ya mwaka wa masomo na tayari fedha hizo zimeshafikishwa katika vyuo husika.

Hadi kufikia leo jumla ya wanafunzi 166,438 wamepangiwa mikopo yenye thamani ya Sh424.5 bilioni kati yao wa mwaka wa kwanza ni 68,460 na wanaoendelea ni 97,978.

Kulingana na Badru wanafunzi wa mwaka wa kwanza wanaolengwa kunufaika na mikopo hiyo kwa mwaka huu ni 71,000.

“Bajeti isingeongezwa ni wazi wanafunzi 28,000 wangekosa mikopo lakini kutokana na hatua hii iliyochukuliwa wataweza kupata ufadhili huu. Hawa waliopata walikuwa tayari wameshafanyiwa tathmini na kuonekana mahitaji yao ni makubwa,”amesema Badru.