CAG aeleza Sh74 milioni zilivyochotwa ujenzi zahanati Kipunguni

CAG atilia shaka malipo ya Sh830 milioni kwa TBC na Clouds

Muktasari:

Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali (CAG),  Charles Kichere amesema katika ukaguzi wake amebaini upotevu wa Sh74 milioni uliosababisha kutokamilika kwa ujenzi wa zahanati katika kata ya Kipunguni jijini Dar es Salaam.


Dar es Salaam. Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali (CAG),  Charles Kichere amesema katika ukaguzi wake amebaini upotevu wa Sh74 milioni uliosababisha kutokamilika kwa ujenzi wa zahanati katika kata ya Kipunguni jijini Dar es Salaam.

Kichere amesema ofisa mtendaji wa kata hiyo na mtia saini wa akaunti ya maendeleo ya kata walihusika na kosa hilo.

Ameeleza hayo katika ripoti yake inayoishia Juni 2020 aliyoichambua leo Alhamisi Aprili 8, 2021 katika mkutano wake na waandishi wa habari mjini Dodoma.

“Mapitio ya jalada IMC/JW.12/1 la maendeleo ya kata ya Kipunguni na daftari la makosa ya kinidhamu yalibaini kuwa ofisa mtendaji wa kata ya Kipunguni na mtia saini wa akaunti ya maendeleo ya kata ya Kipunguni walikutwa na kosa la upotevu wa fedha Sh74,093,000,” amesema Kichere.

Amesema fedha hizo zilitolewa kwa ajili ya ujenzi wa zahanati ya kata ya Kipunguni na hivyo upotevu huo ulisababisha mradi wa ujenzi kutokamilika.