Ehud Barak atua nchini akisifia vivutio vilivyopo
Ngorongoro. Meneja Uhusiano wa Shirika la Hifadhi za Taifa (Tanapa), Pascal Shelutete amesema Waziri Mkuu mstaafu wa Israel, Ehud Barak amekuja nchini kutokana na kuvutiwa na vivutio vya utalii vilivyopo nchini, ikiwamo Hifadhi ya Serengeti yenye idadi kubwa ya nyumbu wahamao.
Akizungumzia ziara hiyo, Shelutete amesema ziara ya kiongozi aliyekuja na familia yake pamoja na watalii wengine zaidi 100, imefungua milango kwa Waisraeli kuitembelea Tanzania.
Amesema ujio za msafara wa kiongozi huyo unaonyesha kwamba Tanzania imejaliwa kuwa na vivutio vingi vinavyohitaji kutembelewa na wananchi pamoja wageni.
Naye Meneja Utalii wa Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro, Paul Fisoo alisema ziara ya Barak inathibitisha utajiri wa vivutio vya utalii vilivyopo nchini.
Awali, waziri mkuu huyo mstaafu alisema Tanzania imejaliwa kuwa na utajiri wa vivutio vya utalii ambavyo havipo katika nchi yoyote duniania.