FAIDA YA MATUNDA NA TIBA MWILINI

Muktasari:

Leo katika dondoo za afya nitakutajia orodha ya juisi zilizotengenezwa kwa matunda na mboga na fadia zake mwilini.

Wote tunafahamu kuwa chakula ni dawa. Chakula unachokula leo ndicho kinachoamua hali yako ya kiafya kesho. Unaweza kuishi bila kuugua kama ukila vyakula vyote muhimu vinavyohitajika mwilini.

Leo katika dondoo za afya nitakutajia orodha ya juisi zilizotengenezwa kwa matunda na mboga na fadia zake mwilini.

Katika orodha hii, utaona kuna mchanganyiko wa matunda au mboga mbili hadi nne na kazi zake mwilini, zikitumika kama tiba au kinga ya magonjwa.

TUFAHA, TANGO NA FIGILI

Ofisa Lishe, Mtafiti, Elimu na Mafunzo ya lishe kutoka Taasisi ya Tiba na Lishe, Walbert Mgeni anatueleza kuwa juisi yenye mchanganyiko wa matunda haya ni kinga dhidi ya saratani, huondoa lehemu (cholesterol) mwilini, husafisha tumbo na pia huondoa maumivu ya kichwa.

KAROTI, TANGAWIZI NA TUFAHA

Ofisa huyo anatueleza kuwa juisi yenye mchanganyiko wa matunda hayo matatu huondoa sumu mwilini na kuimarisha mfumo wa kinga ya mwili. Tufaha ni tunda maarufu ambalo hujulikana huitwa apple kwa Kiingereza.

CHUNGWA, TANGAWIZI NA TANGO

Mgeni anasema juisi yenye mchanganyiko wa matunda haya hung’arisha rangi ya ngozi na kuifanya kuwa laini. Pia hupunguza joto la mwili. Kwa wale wenye matatizo ya kuwa na ngozi kavu, juisi hii itawasaidia sana.

NYANYA, KAROTI NA TUFAHA

Mtaalamu huyu anafafanua kuwa juisi yenye mchanganyiko wa matunda haya hufanya ngozi ya mwili mzima kuwa nyororo na huondoa harufu mbaya mdomoni.

TUFAHA NA TANGO LA KAWAIDA

“Juisi yenye mchanganyiko wa matunda haya huondoa harufu mbaya mdomoni na hupunguza joto la mwili,” anasema Mgeni.

NANASI, TUFAHA NA TIKITIMAJI

Anaendelea kusema kuwa juisi yenye mchanganyiko wa matunda haya hufanya kazi ya kuondoa chumvi nyingi mwilini, husafisha kibofu cha mkojo na figo. Juisi hii ni nzuri kwa wale wenye matatizo ya kibofu na figo au wanaotaka kujikinga na magonjwa hayo.

KAROTI, PEASI, TUFAHA NA EMBE

Mgeni anasema juisi yenye mchanganyiko wa matunda haya huzuia athari ya sumu mwilini, hupunguza shinikizo la damu na kuondoa mlundikano wa uchafu mwilini.

NDIZI, NANASI NA MAZIWA

Hata hivyo anasema juisi hii yenye kiasi kikubwa cha vitamini na virutubisho mbalimbali vyenye faida mwilini, huzuia tatizo la ukosefu wa choo.

Aidha Mgeni anasema ili mtu aweze kupata faida hizo zilizoainishwa katika kundi la matunda hayo, usafi wa matunda yenyewe hauna budi kuzingatiwa wakati wa kutayarisha juisi yake.

“Hakikisha pia unatumia matunda yaliyoiva vizuri na uyatayarishe kwa kuzingatia kanuni ya ‘mtu ni afya’,” anasema.