Hamisa kumlima barua Kajala, meneja wake afunguka

Hamisa kumlima barua Kajala, meneja wake afunguka

Muktasari:

  • Sakata la kuvuja kwa video za mtoto wa Kajala limezidi kuchukua sura mpya baada ya mwanasheria wa mwanamitindo Hamisa Mobeto kumwandikia barua msanii huyo wa filamu.

Dar es Salaam. Sakata la kuvuja kwa video za mtoto wa Kajala limezidi kuchukua sura mpya baada ya mwanasheria wa mwanamitindo Hamisa Mobeto kumwandikia barua msanii huyo wa filamu.
Video hiyo ilivuja jana Jumapili Februari 14, 2021 ambapo inamuonyesha mtoto huyo wa Kajala Masanja akiwa kwenye gari na msanii kutoka lebo ya WCB, Rayvanny wakiwa katika mahaba mazito.
Mwananchi leo Jumatatu Februari 15, 2021 ilifanya mawasiliano na mwanasheria wake Elia Rioba ili kujua walipofikia na kueleza kuwa tayari wameshaandikia barua kwa Kajala ya kumpa maelekezo nini wanataka afanye kwao kutokana na kumchafua mteja wake huyo.
“Kwa taarifa tulizokuwa nazo Kajala bado yupo Zanzibar, ila tayari tumeandika barua kwa ajili yake na mara baada ya kurudi tutamkabidhi ambapo ndani ya barua hiyo kuna maagizo tumeyatoa kwake na kumpa masharti ya nini anapaswa kufanya ndani siku kadhaa na endapo hatayafanya basi tutajua nini cha kufanya,”amesema mwanasheria huyo.
Katika sakata hilo, Kajala ameelekeza tuhuma za aliyesababisha hayo yote kuwa ni mrembo Hamisa Mobeto ambaye naye amechomoa kwa kuandika utetezi mrefu kupitia ukurasa wake kwenye mtandao wa Instagram na kuweka ushahidi wa video juu.
Pia mwanamindo huyo katika ujumbe huo aliapa kulipeleka suala hilo mbele ikiwemo kuwasiliana na mwanasheria wake kuona hatua gani zaidi zitachukuliwa kwa kile alichoeleza kachafuliwa sio tu jina lake katika suala hilo bali na brand yake.
“Mimi ni mama, mfanyabiashara, mdau na balozi wa makampuni mbalimbali, ‘brand’ yangu nimeijenga kwa muda mrefu hivyo ningependa iheshimike na isichafuliwe kwa shutuma za uongo kama hizi,”ameandika Hamisa.
Kwa upande wake Meneja wa Hamisa, Dk Ulimwengu amesema Hamisa Mobeto si tu jina bali ni ‘brand’, hivyo kama meneja wake hatakubali kuona suala hilo linaisha kishkaji ni lazma sheria ifuatwe.
“Hamisa Mobeto ina wafanyakazi, ina wateja wake sasa wakiona inahusishwa na mambo mabaya kama hayo yaliyoonekana huko mitandaoni ni wazi yataharibu biashara ya kampuni, hivyo tusingependa suala hili limalizwe kishkaji, lazima sheria ifuate mkondo wake,”amesema.