Hello

Your subscription is almost coming to an end. Don’t miss out on the great content on Nation.Africa

Ready to continue your informative journey with us?

Hello

Your premium access has ended, but the best of Nation.Africa is still within reach. Renew now to unlock exclusive stories and in-depth features.

Reclaim your full access. Click below to renew.

Hatma ya urais wa Liberia kujulikana leo, George Weah atabiriwa kushinda

Muktasari:

Uchaguzi huo unaashiria mabadiliko ya kwanza ya kidemokrasia tangu mwaka 1944

Monrovia, Liberia. Wananchi wa Liberia leo wanamchagua kiongozi mpya katika uchaguzi wa duru ya pili kati ya Makamu wa Rais Joseph Boakai na mchezaji kandanda wa zamani maarufu, George Weah.

Kura hiyo itaashiria mabadiliko ya kwanza ya uongozi nchini humo tangu mwaka 1944.

Baada ya wiki saba za ucheleweshaji kutokana na malalamiko ya kisheria yaliyofikishwa mahakamani na chama tawala cha Boakai cha Unity dhidi ya tume ya uchaguzi nchini humo, vituo vya kupigia kura vinatarajiwa kufunguliwa kuanzia saa mbili asubuhi saa za Liberia na kufungwa majira ya saa 12 jioni kwa ajili ya wapigakura milioni 2.1 walioandikishwa.

Chama cha Weah cha muungano kwa ajili ya mabadiliko ya kidemokrasi Coalition for Democratic Change (CDC) kiliwataka wapigakura kutokunywa pombe kupita kiasi katika Sikukuu ya Krismasi na kuamka mapema leo kupiga kura katika kile mwenyekiti wa tume ya uchaguzi ya taifa NEC, Francis Korkoya alichosema kuwa ni “kujitolea mhanga kwa ajili ya demokrasia yetu na nchi yetu.”

Wananchi watachagua mrithi wa Rais Ellen Johnson Sirleaf, anayetarajiwa kuondoka madarakani mwezi Januari baada ya miaka 12 akiwa katika uongozi wa juu wa taifa hilo la Afrika Magharibi, linaloibuka kutoka katika mavumbi ya vita vya wenyewe kwa wenyewe,(1989-2003) na pia kushughulikia hatua za kupambana na mzozo wa ugonjwa wa ebola (2014-16).

Katika duru ya kwanza ya upigaji kura iliyofanyika Oktoba 10, Weah alipata asilimia 38.4 ya kura wakati Boakai alikuwa wa pili akipata asilimia 28.8 na kuzusha hatua ya duru ya pili ya uchaguzi kwa kuwa hakuna kati ya wagombea hao wawili aliyeweza kufikisha idadi ya asilimia 50 ya kura inayohitajika kushinda moja kwa moja.

“Matokeo yatakuwa yanakaribiana sana,” amesema Ibrahim Al-Bakri Nyei, mchambuzi wa masuala ya siasa nchini Liberia katika shule ya mitaala ya masuala ya Mashariki ya Kati na Afrika katika Chuo Kikuu mjini London (SOAS).

Amesema kwamba Weah alikuwa katika nafasi kama hiyo katika uchaguzi wa mwaka 2005 wakati aliposhindwa licha ya wengi kutabiri kwamba atashinda. Kutokana na siku ya uchaguzi, “inawezekana kuwapo idadi ndogo ya watu watakaopiga kura kuliko uchaguzi wa kwanza,” alitabiri.

Akisifu mchakato usiokuwa na ghasia wa uchaguzi hadi sasa, Sirleaf alisema katika hotuba yake hivi karibuni kwamba “uchaguzi umechukua nafasi ya risasi na mizozo ya uchaguzi inatatuliwa kupitia mahakama”, ikiwa ni ishara ya umbali gani Liberia imetoka tangu wakati wa vita.

Chama cha Unity cha Boakai kimejiunga na chama cha upinzani cha Liberty kupambana na kile alichosema “mapungufu makubwa na udanganyifu” katika matokeo ya uchaguzi, lakini mahakama kuu iligundua kuwa madai hayo hayakuweza kuthibitishwa na waangalizi walitangaza kuwa uchaguzi huo ni wa kuaminika.

Wakati huohuo juhudi za kuvutia kuungwa mkono kutoka kundi la wagombea wengine 18 walioshindwa katika kinyang’anyiro hicho katika duru ya kwanza imeishia katika kupata wagombea wachache wasio na uhakika licha ya Weah kuidhinishwa na mbabe wa kivita aliyejibadilisha kuwa mchungaji Prince Johnson, ambaye ni maarufu sana katika kaunti yenye wakaazi wengi ya Nimba.

Mwanasoka huyo wa zamani Weah pia alipigwa picha katika tukio la hadhara pamoja na Sirleaf Alhamis, akikoleza uvumi kwamba rais huyo mstaafu anaweza kumuidhinisha dhidi ya makamu wa rais aliyetumika naye kwa miaka 12.

Weah pia alipata kura nyingi katika kaunti ya Bong, ngome ya mbabe wa kivita wa Liberia rais wa zamani Charles Taylor na mkewe wa zamani , Jewel Howard-Taylor, ambaye ni makamu wa rais aliyeteuliwa na mwanasoka huyo wa zamani.

Charles Taylor kwa sasa anatumikia kifungo cha miaka 50 nchini Uingereza kwa uhalifu alioufanya katika nchi jirani ya Sierra Leone, lakini ushawishi wake bado upo katika uchaguzi huo.