Hospitali Rombo kuhudumia watu laki tatu
Muktasari:
- Zaidi ya wananchi 300,000 waliokuwa wakikabiliwa na changamoto ya kutembea umbali mrefu kusaka huduma za afya katika Wilaya ya Rombo.
Rombo. Zaidi ya wananchi 300,000 waliokuwa wakikabiliwa na changamoto ya kutembea umbali mrefu kusaka huduma za afya katika Wilaya ya Rombo, mkoani Kilimanjaro wataondokana na adha hiyo mara baada ya ujenzi wa hospitali mpya ya wilaya ambayo imefikia asilimia 90 ujenzi wake kukamilika.
Mbunge wa Rombo, Profesa Adolf Mkenda amesema Leo Desemba 5 kuwa tayari serikali imeshatoa fedha zaidi ya Sh2.3 bilioni kwa ajili ya ujenzi huo ambao una majengo 10 likiwamo la mama na mtoto,jengo la mionzi na wodi ya wazazi na watoto.
Profesa Mkenda ambaye pia ni Waziri wa Kilimo amesema tayari amezungumza na mkurugenzi wa halmashauri pamoja na mhandisi anayetekeleza mradi huo kuongeza kasi ya ujenzi huo ili wananchi waweze kupata huduma mapema katika Hospitali hiyo.
"Leo nimekuja kutembelea hospitali hii ya wilaya inayojengwa hapa eneo la kiwanda,Kirongo Samanga kuangalia maendeleo ya ujenzi na kutambua changamoto zilizopo.Tunaishukuru serikali kutoa Sh2.3 bilioni kwa ajili ya hospitali hii,na sasa hivi tayari tuna Sh1.39 bilioni ambazo zimekuja tena kwa ajili ya kuendeleza ujenzi huu,"amesema Profesa Mkenda
"Hospitali hii itakapokamilika itaondoa changamoto kwa wananchi kutembea umbali mrefu kutafuta huduma za afya. Changamoto iliyopo kwa sasa ni barabara lakini tumeshaiweka katika utaratibu wa Tarura,bajeti yake imetoka kwa hiyo itatengenezwa ili wananchi waweze kufika hapa kirahisi kwa ajili ya kupata huduma mbalimbali za matibabu,"amesema Profesa Mkenda
Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo,Gilbert Tarimo amesema ujenzi wa hospitali hiyo ulioanza mwaka 2019 utakapokamilika itaweza kuhudumia zaidi ya wananchi 300,000 ambao walikuwa wakitafuta huduma katika meneo mbalimbali ndani na nje ya Rombo.
"Tunashukuru serikali yetu kwa ajili ya kutenga maeneo na kujenga hospitali hii ambayo itatumika kuhudumia wananchi wote wa Rombo zaidi ya 300,000 kwani walikuwa wakipata adha kubwa ya kutafuta huduma za afya wakati mwingine nje ya Rombo ,"alisema Tarimo
Nao baadhi ya wananchi wa wilaya hiyo wakamshukuru Rais Samia kwa kupeleka huduma hiyo ya hospitali katika wilaya hiyo kwani walikuwa wakipata adha ya huduma za afya kutokana na hospitali pamoja na vituo vingi vya afya vilivyopo wilayani humo kuwa ni vya watu binafsi.
"Rais Samia ametutendea haki sisi wananchi wa Rombo,tunamwombea kwa Mwenyezi Mungu ampe afya njema ili aweze kulipigania Taifa hili ,tunashukuru sana kwa ujenzi wa hospitali hii tunaamini itakapokamilika wananchi ambao ni wanyonge tutapata unafuu wa maisha katika kutibu afya zetu,"alisema Maria Mlingi mkazi wa kijiji cha Kiwanda ,kata ya Kirongo Samanga.