Kidato cha kwanza 2022 wote kuanza shule siku moja

Kidato cha kwanza 2022 wote kuanza shule siku moja

Muktasari:

  • Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-Tamisemi, Ummy Mwalimu  amesema wanafunzi watakaochaguliwa kuanza kidato cha kwanza mwakani wote wataanza shule siku moja tofauti na ilivyokuwa miaka ya nyuma.

Dar es Salaam. Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Ummy Mwalimu amemuhakikishia Rais Samia Suluhu Hassan kuwa wanafunzi watakaofaulu na kuchaguliwa kujiunga kidato cha kwanza mwakani wote wataanza shule siku moja.

Ummy amesema hayo leo Jumatatu Septemba 27, 2021 katika mkutano mkuu maalumu wa uchaguzi viongozi wa Jumuiya ya Tawala za Mitaa Tanzania (ALAT) ngazi ya Taifa unaofanyika mkoani Dodoma.

Amesema amepata maagizo kutoka kwa kiongozi huyo kupitia Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa kuwa asingependa kuona mwakani wanafunzi wanapishana kuanza shule kwa kisingizio cha uhaba wa madarasa.

“Ujumbe wako Rais nimeupata, hakuna cha kusubiri, madarasa lazima tuyajenge na nikuhakikishie tayari tumeshaanza kuyafanyia kazi, na wanafunzi wote itakapofika siku ya kufungua shule Januari 6, wote wataanza kwa pamoja, hakuna cha wa kwenda baada ya kusubiri miezi miwili au mitatu ili tumalize madarasa,” amesema Waziri huyo.

Alimshukuru Rais Samia kwa kuendeleza sera ya elimu bila ada, kwani katika miezi yake miwili ya bajeti yake ya kwanza ya mwaka 2021/22  wameshapeleka kwenye halmashauri zote 84 Sh62.4 bilioni.

“Tunakushukuru Rais, kwani kulikuwa na uzushi kwamba elimu bila malipo itafutwa chini ya uongozi wako lakini wote ni mashahidi fedha zimeshakwenda katika halamshauri zetu katika shule zetu za msingi na sekondari.

“Katika hili tunakushukurum, umesaidia watoto wa maskini kupata elimu,”amesema Ummy.

Kutokana na sera hiyo ya elimu bila malipo, Waziri huyo amesema wanafunzi wanaotarajiwa kuanza  kidato cha kwanza ni takribani milioni moja wakati wanafunzi wanaomaliza kidato cha nne ni 460 kwa hiyo kuna ongezeko la wanafunzi wa kidato cha kwanza zaidi ya 500.