Kigwangalla kupinga kortini ujenzi wa Makao Makuu Nzega

Kigwangala kupinga kortini ujenzi wa Makao Makuu Nzega

Muktasari:

  • Wakati Waziri Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Innocent Bashungwa akielekeza Makao Makuu ya halmashauri ya Wilaya ya Nzega Vijijini yajengwe Lubisu badala ya Ndalla, Mbunge wa Nzega Vijijini, Dk Hamisi Kigwangalla, amesema atakwenda mahakamani kupinga agizo hilo.

Tabora. Wakati Waziri Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Innocent Bashungwa akielekeza Makao Makuu ya halmashauri ya Wilaya ya Nzega Vijijini yajengwe Lubisu badala ya Ndalla, Mbunge wa Nzega Vijijini, Dk Hamisi Kigwangalla, amesema atakwenda mahakamani kupinga agizo hilo.

Wiki iliyopita Waziri Innocent Bashungwa aliwaita viongozi wa halmashauri ya Wilaya ya Nzega Vijijini Jijini Dodoma na kuwaeleza eneo linalotakiwa kujengwa makao makuu ya halmashauri.

Miongoni mwa viongozi waliofika katika kikao cha Waziri Bashungwa ni pamoja na Dk Kigwangala, Mwenyekiti wa Halmashauri Henerico Kanoga na Mkurugenzi wa halmashauri hiyo, Kiomoni Kibamba.

Akizungumza na wakazi wa Tarafa ya Puge katika kata ya Ndalla jana Februari 21, Kingwangalla amesema mchakato, sheria na kanuni hazijafuatwa na wala nguvu ya hoja haijaangaliwa katika kuamua sehemu ya kujengwa Makao Makuu ya halmashauri.

Amesema kwa kuwa pesa nyingi zimetumika kuyaweka kwa muda makao makuu eneo la Ndalla na sasa wanabadilisha kwenda eneo jingine lazima wapiganie uamuzi wa awali ambayo tayari ulianza kutekelezwa ya kujengwa eneo la Ndala.

“Pale inapobidi kupambana nitafanya hivyo kwa masilahi ya wananchi na sio masilahi yangu binafsi," amesema

Amewaeleza wakazi wa Ndala kuwa tayari amemuandikia barua Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa kuhusu suala hilo na amemuomba aunde timu ya kuangalia mchakato mzima ulivyokwenda na kisha aelekeze namna ya kufanya.

Amesema wakati wanasubiri maelekezo ya Waziri Mkuu, amemuomba Mkuu wa Mkoa, Dk Baltida Burian kusitisha mchakato wa ujenzi wa makao makuu mapya ya halmashauri eneo la Lubisu hadi pale yatakapotoka maelekezo ya Waziri Mkuu.

Amemtaka pia Dk Batilda kuielekeza Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), kuchunguza tuhuma za baadhi ya madiwani kupewa rushwa ya Sh70,000 ili wabadili maamuzi ya ujenzi wa makao makuu mapya.

Amemtaka pia aielekeze TaKukuru kuchunguza kama wananchi wa eneo hilo jipya wanachangishwa Sh19,000 kwa ajili ya kupata fedha za kulipa watu fidia na pia kuielekeza TaKukuru kumchunguza kama ana eneo Ndalla kama anavyozushiwa kuwa nalo na ndio maana anang'ang'ania Makao Makuu yawe Ndala.

Dk Kigwangalla amesema anapambana kutafuta haki na ukweli kamwe hauwezi kushindwa na hatua zote zikishindikana ataenda mahakamani kupinga kuanza ujenzi katika makao makuu mapya ili kupata haki.

Naye Diwani wa Kata ya Ndala, Ramadhani Chimani amesema zaidi ya viwanja 2,400 vimepimwa katika eneo la Ndalla na watu walikuwa wameanza kuwekeza lakini sasa hawajui hatima yao.

Amesema Baraza la madiwani lilikubaliana makao makuu yajengwe Ndala lakini imetokea sintofahamu na wananchi kubaki gizani.

Hata hivyo, Mwenyekiti wa halmashauri ya Wilaya ya Nzega Vijijini, Henerico Kanoga amesema wameshapata kibali cha ujenzi na muda wowote kazi itaanza.

Amesema wanafuata maelekezo ya Serikali ambayo yameelekeza Makao Makuu yajengwe eneo hilo na sio Ndala jambo ambalo wameridhia.

"Serikali tayari imetoa maelekezo yake kuhusu ni sehemu gani ya kujengwa makao makuu ya halmashauri yetu na sisi tunafuata kwani huwezi kubishana na Serikali," amesema.

Kuhusu Dk Kigwangalla kwenda mahakamani kupinga ujenzi wa Makao Makuu eneo jipya, amesema aende kwa kuwa wao hawawezi kumzuia lakini wao wanazingatia maelekezo ya Serikali.