Kijana aua wanafunzi 19, walimu wawili

Muktasari:

  • Wanafunzi 19 na waalimu wawili wamefariki dunia kwa kupigwa risasi baada ya mtu mmoja kufanya shambulizi katika shule ya msingi kusini mwa Texas nchini Marekani.

Texas, Marekani. Wanafunzi 19 na waalimu wawili wamefariki dunia kwa kupigwa risasi baada ya mtu mmoja kufanya shambulizi katika shule ya msingi kusini mwa Texas nchini Marekani.

Maofisa wa usalama wamesema kuwa mshambuliaji huyo mwenye umri wa miaka 18 alifyatua risasi katika shule hiyo kabla ya kuuawa na polisi.

Taarifa zinasema kuwa mtuhumiwa huyo alikuwa amejihami kwa bunduki yenye uwezo wa juu.

Kabla ya kufanya shambulizi hilo katika shule hiyto, kijana huyo anadaiwa kumpiga risasi bibi yake.

Vyombo vya habari nchini humo vimeripoti kuwa huenda alikuwa mwanafunzi wa shule ya upili katika eneo hilo.

Mkuu wa Polisi wa mji wa Uvalde ambako shule hiyo ilipo, Pete Arredondo amesema mauaji hayo yalifanyika Jumanne Mei 24, 2022 na kwamba kijana huyo alifanya shambulizi hilo peke yake.

Gavana wa Texas, Greg Abbott amesema mshambuliaji huyo aliacha gari nje kabla ya kuingia shuleni na kufyatua risasi.