Kikwete aonya kuchanganya dini na siasa

Rais wa awamu ya nne, Jakaya Kikwete. Picha na Maktaba

Muktasari:

  • Rais Mstaafu wa awamu ya nne, Jakaya Kikwete amewaonya viongozi wa dini na siasa kutumia dini kwa manufaa yao huku akisema ni hatari kwa amani ya nchi.

Dar es Salaam. Rais Mstaafu wa awamu ya nne, Jakaya Kikwete amewaonya viongozi wa dini na siasa kutumia dini kwa manufaa yao huku akisema ni hatari kwa amani ya nchi.

Kikwete ameyasema hayo leo Jumapili Agosti 20, 2023 katika uzinduzi wa Kanisa la Waadventista Wasabato Charya Kamageta wilayani Rorya mkoani Mara.

"Natumia nafasi hii kukumbusha kuhusu tunu nyingine muhimu nayo ni kutokuchanganya dini na siasa tukiivunja tunu hii gharama yake tutaiona, kama kuna viongozi wa dini wanaotaka kutuelekeza kuitumia dini kwa manufaa ya kisiasa na kama kuna Viongozi wa siasa wanataka kuitumia dini kwa manufaa yao ya kisiasa nawaombeni tuwanyanyapae,”amesema Kikwete.

Kikwete amesema athari ya kuchanganya dini na siasa ni uvunjifu bwa amani na utulivu wa Taifa.

“siku ikifika uwanachama wa chama cha kisiasa au uumini thabiti wa dini ukawianishwa na chama cha kisiasa anachokifuata ndiyo mwisho wa nchi yetu.

“kutakuwa na chama cha siasa cha wakristo, cha waislamu vyama vya siasa vya walokole. Kuwafanya Watanzania kuyatazama masuala ya kisiasa, Serikali na utawala kwa mtazamo wa  dini zetu ni jambo hatari,”amesisiza

Pia amesema watu kuyatazama mambo ya kidini kwa mtazamo wa siasa na vyama vyao si jambo lenye afya kwa Taifa huku akieleza yote mawili yataathiri umoja na kutishia amani, usalama na utulivu wanaoufaidi hivi sasa.

Kikwete ameyasema hayo ikiwa ni siku mbili tangu Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC)  kutoa tamko lake kuhusu mkataba wa uwekezaji wa Bandari kati ya Serikali ya Tanzania nay a Dubai ambao ulipitishwa na Bunge la Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Jumamosi Juni 10, 2023.