Mageuzi ya sekta ya kilimo nchini kupitia ujengaji uwezo wa kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi

  • Ofisa Mtendaji Mkuu na mmiliki wa kampuni ya Jackama Enterprise, Jackson Massawe akikagua mshine ya kujazia mafuta ya alizeti iliyopo kwenye kampuni yake jijini Dodoma. Picha na SNV- CRAFT-2020.

Muktasari:

  • Kilimo ni moja ya sekta muhimu zaidi Afrika Mashariki, huku asilimia 80 ya wakazi wa ukanda huo wanaishi katika maeneo ya vijijini na maisha yao yanategemea shughuli hiyo kwa kiasi kikubwa na taarifa hiyo ni kulingana na Jumuiya ya Afrika Mashariki (2019).Ifa­hamike kuwa, sekta ya kilimo ndiyo inayoendesha sehemu kubwa ya uchumi wa Tanzania.

Kilimo ni moja ya sekta muhimu zaidi Afrika Mashariki, huku asilimia 80 ya wakazi wa ukanda huo wanaishi katika maeneo ya vijijini na maisha yao yanategemea shughuli hiyo kwa kiasi kikubwa na taarifa hiyo ni kulingana na Jumuiya ya Afrika Mashariki (2019).Ifa­hamike kuwa, sekta ya kilimo ndiyo inayoendesha sehemu kubwa ya uchumi wa Tanzania.

Kulingana na Benki Kuu ya Tanzania (2018), sekta ya kili­mo inachangia kwa asilimia 30 ya Pato la Taifa na kwa ukubwa huo sekta ya kilimo ni mara tatu ya ukubwa wa sekta ya biashara kwa asilimia 11, madi­ni kwa asilimia 4.8, na uzalish­aji wa viwanda kwa asilimia 5.5.

Sekta hiyo inaajiri takriban asilimia 77.5 ya nguvu kazi ya nchi na inachangia zaidi ya asilimia 95 katika mahitaji ya kitaifa ya chakula ukirejelea Mpango wa Maendeleo ya Sekta ya Kilimo II-ASDP II wa mwaka 2017.

Kwa Afrika Mashariki yote, mabadiliko ya tabianchi na kutokutabirika kwa hali ya hewa huathiri kiasi kikubwa uzalishaji wa kilimo, mifumo ya chakula na usalama wa chakula.

  • Amina Matata wa Kijiji cha Jenjeluse jijini Dodoma hufanya kilimo bora kutumia mafunzo aliyopata katika Mradi wa Kilimo Himilivu kulingana na tabianchi kwa siku za usoni (CRAFT). Picha na SNV- CRAFT-2020.

Utafiti umegundua kuwa mabadiliko ya hali ya hewa yana athari tofauti kwa mae­neo tofauti ya kijiografia na mwenendo wa mazao, na idadi ya watu walio katika mazingira magumu wako katika uweze­kano mkubwa wa kuathiriwa zaidi. Vilevile, kuongezeka kwa idadi ya watu mijini Afri­ka kunasababisha mahitaji ya chakula kuongezeka.

Hii inachagiza haja ya kuund­wa kwa njia jumuishi, ambayo imekuwa ikifahamika kama ‘utumiaji na uongezaji masu­luhisho na mbinu za kisasa za kukabiliana na mabadiliko ya hali ya hewa na tabanchi kwa ujumla kwa ajili ya maendeleo endelevu na jumuishi ya kilimo cha kibiashara.’

Kwa kuwa kilimo kinatege­mea mvua kwa kiasi kikubwa na rahisi kuathiriwa na mab­adiliko ya tabianchi na kuto­kutabirika kwa hali ya hewa, athari hasi za mabadiliko ya tabianchi tayari zinaonekana katika mifumo ya kilimo kwa Afrika Mashariki kupitia vipin­di vikali vya hali ya hewa, mab­adiliko ya mipaka ya ikolojia ya kilimo, kupungua kwa ubora wa mazao na wingi, na ongezeko la magugu na wadudu.

Mradi wa Kilimo Himilivu kulin­gana na tabianchi kwa Siku za Usoni (CRAFT)

Mradi wa Kilimo Himil­ivu kulingana na tabianchi kwa Siku za Usoni (CRAFT) ulianzishwa mahususi kwa ajili ya kushughulikia changamoto hizi zinazohusiana na mabadi­liko ya tabianchi zinazoathiri sekta ya kilimo kwa nchi za Kenya, Tanzania na Uganda.

Mradi huu wa miaka mitano, uliozinduliwa mwaka 2018, chini ya ufadhili wa Wizara ya Mambo ya nje ya Uholan­zi, unatekelezwa na Shirika la Maendeleo la Uholanzi la SNV kwa kushirikiana na Chuo Kikuu cha Wageningen na Utafiti, Programu ya Utafiti ya CGIAR juu ya Mabadiliko ya Tabianchi, Kilimo na Usalama wa Chakula, Agriterra, na Ush­irikiano wa Rabo.

CRAFT inafanya kazi kupitia kwa sekta binafsi, na inasaid­ia wadau wa sekta ya umma katika kutengeneza mazingira wezeshi uliojikita katika usha­hidi wa mashambani kwa utu­miaji wa kiwango kikubwa wa Njia za Kilimo Stahamilivu na cha Kisasa (CSA), pamoja na matumizi bora, yenye tija ya nishati mbadala katika kilimo.

Shughuli za CRAFT zimehu­sishwa katika uwekezaji jumui­shi na kukabiliana na mabadi­liko ya tabianchi ili kuimarisha mienendo ya kilimo biashara na ushirika katika minyororo saba ya thamani nchini Ugan­da, Kenya na Tanzania.

Kiongozi wa Sekta ya Kilimo kutoka shirika la SNV hapa nchini, Menno Keizer anasema kuwa, “Gharama ya kutofanya chochote inaweza kuwa juu zaidi mara 20 ikilinganishwa na ile ya kutowekeza katika hatua za kukabiliana na mab­adiliko ya hali ya hewa.”

Mkakati wa utekelezaji unat­egemea hatua za ziada katika ngazi tatu: (a) mifumo ya kili­mo, (b) mifumo ya soko jumui­shi, na (c) mazingira wezeshi. Na faida za utekelezaji wake ni kama ifuatavyo:-

Kuongeza kipato kwa waku­lima wadogo na wajasiriamali wadogo na kati. Hii itafanikiwa kupitia kuongezeka kwa matu­mizi ya mbinu na teknolojia za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi miongoni mwa waku­lima wadogo, wajasiriamali wadogo na kati na vyama vya ushirika.

Pia unaongeza ufanisi wa kibiashara kwa wajasiriamali wadogo na kati wanaofanya kilimo biashara na ushirika kutokana na uwekezaji unaohusiana na udhibiti wa mab­adiliko ya tabianchi. Hili lita­fanikiwa kupitia kuongezeka kwa uwekezaji na ukuaji wa biashara katika minyororo ya thamani kwa muktadha wa hali ya hewa, na kuongezeka kwa ushirikishwaji wa maendeleo ya kilimo biashara ya wan­awake na vijana.

Kuboresha mazingira yanay­owezesha kufanyika kwa kili­mo stahamilivu katika uwanda mpana. Pia hili nalo litaweza kufanikiwa kwa kuongezeka kwa ushirikiano na ubadilis­hanaji uzoefu kati ya wadau wa sekta ya umma na binafsi katika utekelezaji wa kilimo stahamilivu.

Mafanikio ya mradi wa CRAFT katika sekta ya kilimo nchini kwa kipindi cha miaka 3 iliyo­pita

i. Mradi ulisaidia wakulima wadogo 37,500 (asilimia 40 wakiwa ni wanawake) kupata maarifa na ujuzi katika kuk­abiliana na mabadiliko ya hali ya hewa na masuluhisho ya udhibiti kama matumizi ya mbegu zilizoboreshwa, udhibi­ti wa udongo na maji pamoja na utunzaji wa mashamba baada ya mavuno. Hii imesababisha mavuno na mapato kuimarika mara dufu.

ii. Kupitia Mfuko wa Ubunifu na Uwekezaji kwenye masuala ya tabianchi (CIIF), CRAFT imewekezaa zaidi ya Pauni 2.6 Milioni katika uwekezaji wa uondoaji hatari kwa wafanya­biashara 18 wa kilimo biashara na ushirika nchini; na hivyo kuchochea matumizi ya njia na teknolojia za kisasa za kilimo stahamilivu katika minyororo maalumu ya thamani ya chaku­la kama alizeti, viazi, maharag­we na mtama.

iii. Ili kuhakikisha kunakuwa­po ujumuishaji wa kijinsia na vijana, makampuni yapatayo 6 ya kilimo biashara yanaongoz­wa au kumilikiwa na wanawake na vijana.

iv. Katika juhudi za kupun­guza uzalishaji wa gesi ya ukaa kutoka katika shughuli za kilimo biashara, mradi huo ulisaidia matumizi ya nisha­ti mbadala na namna bora ambayo nishati hizo zinat­akiwa kutumika katika kilimo biashara. Lengo hili lilifanikiwa kupitia uhamasishaji, upangaji wa maonyesho ya teknolojia na msaada wa maendeleo ya shu­ghuli za kilimo biashara zilizot­hibitishwa na mradi.

v. Kupitia Tathmini ya Hatari ya Hali ya Hewa ya nchi kwe­nye minyororo ya thamani mahususi(CRA),hatari ya mabadiliko ya tabianchi na mikakati inayofaa ya kukabili­ana nayo kwa wadau tofauti tofauti, rasilimali na michakato katika minyororo ya thamani iliyowezeshwa ya mradi, ilit­ambuliwa nchini. Matokeo ya uchambuzi yalitumika kuhui­sha miongozo ya mazao na kuandaa masimulizi ya hali ya hewa na biashara.

vi. Kuhamasisha na kukuza uimara wa kaya kwa kuzinga­tia mabadiliko ya tabianchi, kwa kuwezesha mashamba darasa yanayozingatia mbinu na teknolojia ya kilimo himil­ivu. Pamoja na, mafunzo ya usimamizi wa kifedha na uta­maduni wa kuweka akiba kati ya wakulima wadogo na shu­ghuli za kilimo biashara. Hii iliwawezesha wakulima kud­hibiti majanga na mafadhaiko yanayosababishwa na sababu zinazohusiana na mabadiliko ya tabianchi.

vii. Kulifanyika zoezi la Tath­mini ya Hatari ya Hali ya Hewa (CRA). Katika mradi wa CRAFT, mbinu ya tathmini ya hatari ya hali ya hewa (CRA) inachungu­za ni hatari gani wadau tofauti, rasilimali, na michakato katika mnyororo wa thamani inak­abiliana nazo, na kutambua mikakati inayofaa ambayo ita­saidia kupunguza hatari hizi.

Wakati huo huo, elimu iliy­opatikana kutoka katika tath­mini ya CRA inatoa sababu ya kuwapo kwa uendelezwaji wa shughuli za kilimo biashara cha kisasa na himilivu katika mradi wa CRAFT.

Ili kuelewa kutokutabirika kwa hali ya hewa, mifano ya utabiri wa hali ya hewa iliten­genezwa kwa kila zao lililoku­wa katika minyororo ya tha­mani nchini.

Makadirio ya mabadiliko ya hali ya hewa yalifanywa kwa matukio tofauti tofauti katika minyororo ya thamani iliyot­ambuliwa.

Kwa kila mnyororo wa tha­mani, mfano wa majira kama ya mvua, kiwango cha juu, kiwan­go cha chini, na joto la wastani vilichanganuliwa kugundua hatari ya hali ya hewa iliyopo na kupendekeza mikakati inay­ofaa ya kukabiliana kwa ajili ya wadau tofauti, rasilimali na michakato kwa minyororo ya thamani ya mazao yote ya viazi, mtama, maharagwe, na alizeti.

viii. Mfano kama ilivyo mifa­no mingine mingi ya makadirio ya hali ya hewa ililinganisha wastani wa joto la kipindi cha 1961 – 2005 dhidi ya mvua na mwenendo wa joto la baadaye la miaka ya 2050.

Warsha ya CRA yalithibiti­sha makadirio ya hali ya hewa yalionyesha kuongezeka kwa joto la Tanzania kwa nyuzijoto 2 za Celsius (ºC) katika kipindi cha miaka 30 ijayo.

Kwa mfano, katika maeneo yanayolima alizeti, mfano wa makadirio ya hali ya hewa kati­kati ya karne (yaani miaka ya 2050) ulionyesha kuwepo kwa ongezeko la joto kwa karibu nyuzijoto 2.8ºC na 2.5ºC kati­kati, kusini, na mashariki mwa nchi kwa vipindi vyote vifupi (Oktoba, Novemba, Desemba) na virefu (Machi, Aprili na Mei) vya misimu ya mvua. Mvua ya wastani ya msimu pia ilitabiri­wa kuongezeka hadi asilimia 10, hususan katika msimu mre­fu wa mvua.

Vivyo hivyo, idadi ya siku za mvua mfululizo kwa seh­emu ya Kaskazini-Mashariki mwa Tanzania ilikadiriwa kuongezeka kwa asilimia 5-10, ambayo ni siku moja. Licha ya ukweli kwamba, nchi nzima ilikadiriwa/kuonyesha uwepo wa upungufu wa vipindi virefu zaidi ya mvua.

Kwa upande mwingine, mvua katika maeneo ya kaskazini mashariki yanayolima viazi ilikadiriwa kuongezeka kwa asilimia 20-30 katika miaka ya 2030 na 2050; na kupungua kidogo (kwa asilimia 5-10) katika maeneo yanayo­lima viazi Kusini-Magharibi, hususan katika msimu mfupi wa mvua.

Menno Keizer anasema kuwa, “Ikiwa hakuna hatua zin­azoweza kuchukuliwa, athari za mabadiliko ya hali ya hewa kwa mavuno ya mazao nchini Tanzania itaendelea kuwa mbaya sana.”

Analeza kuwa CRAFT ime­wapa jawabu la kutumainiwa la namna ya kukabiliana na hatari za mabadiliko ya tabian­chi na ushiriki wa dhati wadau wa kilimo biashara, wakulima wadogo, Serikali, watunga sera na wadau wengine muhimu kama vyombo vya habari, kupitia chaguo sahihi la njia na mikakati inayokwenda sambamba dhidi ya hatari ya mabadiliko ya tabianchi ya sasa na ya baadaye na kujenga minyororo endelevu ya thamani ya chakula ambayo instahamili hatari ya mabadiliko ya tabi­anchi.

Matokeo ya CRA, kwa mra­di ambao umesaidia wakulima wadogo na shughuli za kilimo biashara, umekuwa na umuhimu mkubwa na faida kwa upangaji mzuri wa shu­ghuli za kilimo (kwa kutumia kalenda ya kisasa ya upan­daji wa mazao), ikiwasaidia kupanga vizuri, kupunguza gharama na kuongeza mavuno na faida.

Kwa mfano, taarifa hii inawasaidia aidha waamue au waache kupanda, wakati gani watamwagilia au la, wakati gani wa kutumia mbolea na upi la na ikiwa wataanza kuvuna au la.

“Kuongezeka kwa mwenen­do mzuri wa kilimo biashara na ushirika. Kupitia Mfuko wa Ubunifu na Uwekezaji kwenye masuala ya tabianchi (CIIF), CRAFT-imewafikia wafanyabi­ashara 18 wa kilimo na ushirika na kuwekeza zaidi ya TZS 6.7 bilioni na kupelekea makampu­ni ya kilimo na vyama vya ushirika viliwekeza zaidi ya TZS bilioni 8.92 katika minyororo maalum ya thamani ya chaku­la,” anaongeza Menno Keizer.

Uwekezaji wa pamoja kupitia mfuko wa CIIF, haujaboresha tu utendaji wa kilimo biashara pekee ambapo 33 aidha zina­ongozwa au kumilikiwa na wanawake / vijana) lakini pia imeongeza uimara wa kukabili­ana na majanga yanayohusiana na mabadiliko ya tabianchi.

Kwa kuongezea, kupitia CIIF, makampuni hayo yameanzi­sha uhusiano wa kibiashara na wazalishaji kupitia kilimo cha mkataba shirikishi ambayo sio tu iliimarisha mnyororo wa ugavi wa kampuni lakini pia iliongeza mapato ya wakulima kwa kuuza mazao yao kwa bei nzuri. Baadhi ya kampuni za Kili­mo zilizonufaika na mradi wa CRAFT;

Mradi huo mkubwa umeku­wa na manufaa makubwa kwa jamii na kila aliyeshiriki. Kam­puni tatu za kilimo biashara za Temnar, Nondo na EAFFC ndiyo miongoni mwa wanau­faika hao, ambazo kupitia hizo, mradi wa CRAFT ulifanikiwa kuwafikia wakulima wadogo katika maeneo mbalimbali.

Temnar yenyewe ni kampuni ya kilimo inayohusika na usin­dikaji, usambazaji, na uuzaji wa mafuta ya kula pamoja na alize­ti, Nondo Investment Company ikiwa ni kampuni inayojishu­ghulisha na mnyororo wa tha­mani wa zao la alizeti, na East African Fruit and Farm Com­pany ambayo inajishughulisha na usindikaji, usambazaji, na uuzaji wa zao la viazi.

EAFCC

Mratibu wa mradi kutoka EAFFC, Hance Melchior anas­ema moja ya mafanikio ya CRAFT ni ujuzi walioupata wa kutumia njia za kidijitali kue­ndesha shughuli zao. “Tuna mfumo maalumu wa kusajiri wakulima na mazao yao, pia tunasajiri masoko yaani kuwa­pa wateja fursa ya kuagiza kutoka kwa wazalishaji ambao ndiyo wakulima,” aneleza Mel­chior.

Pia anaeleza kuwa wana mfumo wa kuhifadhi taar­ifa za wakulima kuanzia nini wamelima? Wamevuna nini? Wamevuna kwa kiasi gani? Wameuza wapi?

Mkulima kutoka Rungwe, Moshi, Evarist anasema kuwa, “tulikuwa tayari kukubali mabadliko na kutumia njia za kisasa na himilivu za kilimo kama vile kalenda ya mazao na taarifa za hali ya hewa zime­tusaidia kwa kiasi kikubwa. Mimi kwa sasa ninavuna mpa­ka gunia 120 za viazi mwaka huu ikilinganishwa na gunia 70 mwaka jana kwa sababu ya kufata kalenda ya mazao inayoendana na utabiri wa hali hewa.”

Nondo

Mkurugenzi Mtendaji wa Nondo Investment Company, Herymathew Raymond anase­ma kuwa licha ya faida mbalim­bali zilizopatikana kutokana na kushiriki katika mradi wa CRAFT, alikabiliana na chan­gamoto kubwa ya mabadiliko ya kisera baada ya Serikali kutaka mazao yote kuuzwa kwa mfumo wa stakabadhi ghalani tofauti na hapo awali, jambo ambalo liliathiri kiasi kikubwa kampuni hiyo. “Sera ile ilikuja kutumaliza kwani hatukuweza kununua alizeti tena kutoka kwa wakulima, ilitulazimu tuzifuate mnadani.”

Raymond hata hivyo, anakiri kuwa kampuni yake imefanya kazi kubwa ya kutengeneza soko kwa wakulima wa alizeti kwani kampuni hiyo ina kiwan­da kikubwa cha kukamua alize­ti chenye uwezo wa kukamua alizeti tani 3o (ambayo ni sawa na magunia 500 ya alizeti kwa siku).

Temnar

Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Temnar yenye makao makuu yake Mtwara, John Julius anasema kuwa ili kufikia idadi kubwa ya waleng­wa na kutimiza malengo ya CRAFT, kama kampuni iliingia katika ubia na Mamlaka ya Hali ya Hewa (TMA) ambapo kupi­tia mtaalamu wake aliyeopo katika Kituo cha Utafiti wa Kilimo cha Naliendele (NARI) aliweza kutembelea vikundi vya wakulima vilivyo chini ya Temnar takriban 145 na kutoa mafunzo ya namna ya kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, kulima kisasa na kwa tija. “Pia, mtaalamu huyu alikuwa anatoa mafunzo jinsi ya kutumia na kufasiri taarifa za hali ya hewa kwa ajili ya kuanza msimu ya kilimo.”

Naye kwa upande wake, mkulima wa alizeti na mkazi wa kijiji cha Ngalole, kilicho­po Masasi, Mtwara, Hamida Lucas anasema kuwa, “tuliku­wa tunalima kwa mazoea kwa kuamini kupanda ni mwezi Desemba, lakini baada ya mafunzo ya mradi wa CRAFT mambo yamebadilika. Tumeji­funza kuwa mvua inaponyesha kubwa tukate majani na kutan­daza chini kwani hata inapoka­ta majani yanahifadhi unyevu kwa ajili ya uoteshaji alizeti. Na tumeshauriwa aina ya mazao yanayotakiwa kulimwa katika kipindi ambacho hakuna mvua na mafunzo hayo yamesaidia kuongeza mavuno yetu.”

Matarajio ya baadaye

Kwa miaka ijayo, CRAFT inakusudia kubuni mifumo zaidi ya kuongeza matumizi ya njia na teknolojia za kisasa za kilimo himilivu kwa wakulima wadogo, wajasiriamali na vya­ma vya ushirika, na kuzalisha mazao zaidi na ramani maalum zinazoonyesha maeneo yanay­ofaa kwa minyororo lengwa ya thamani katika kipindi cha mabadiliko ya tabianchi katika miaka 30 ijayo.

Shukrani

Shukurani zetu zinakwenda kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania haswa Wizara ya kilimo, Tamisemi kupitia halmashauri za mkoa na wilaya ambapo mradi wa CRAFT unafanya kazi na mashirika mengine ya umma na serikali.

Wasiliana nasi:

Kwa habari zaidi, tafadhali wasiliana na SVN / CRAFT Tanzania kupitia [email protected].