Magufuli awaonya viongozi wa dini wasiolitakia mema taifa

Askofu wa kanisa Catholic jimbo la Tanga, Anthony Banzi akisalimiana na Mkuu wa Wilaya ya Tanga, Thobias Mwilapwa mara baada ya kuwasili jimboni tayari kwa kuanza ibada ya jubilee ya miaka 25 ya utumishi wake katika jimbo hilo.mgeni rasmi ni Waziri wafts Ummy mwalimu kwa niaba ya Rais John Magufuli

Muktasari:

Anthony Banzi ameadhimisha Jubilee ya miaka 25 ya Uaskofu wa Jimbo Katoliki la Tanga nchini Tanzania huku Rais wa nchi hiyo, John Magufuli akitumia fursa hiyo kusema Serikali anayoiongoza itaendeleza ushirikiano na taasisi za dini huku akionywa wale viongozi wa dini wasiolitakia mema taifa hatowavumilia.


Rais John Magufuli amesema hatawavumilia watakaotumia mwanya wa heshima ya viongozi wa dini kuvuruga amani na umoja wa Taifa la Tanzania huku akiahidi kutoa ushirikiano wa hali na mali kwa viongozi wa madhehebu yote ya dini nchini

 

Tanga. Rais wa Tanzania, John Magufuli amesema Serikali anayoiongoza itahakikisha inawaunga mkono viongozi wa dini katika utekelezaji wa majukumu yao ya kuwalea kiroho wananchi kwa sababu mchango wao ni mkubwa katika kuimarisha amani ya nchi.

Hata hivyo, amesema hatawavumilia  baadhi ya viongozi wa dini wasiolitakia mema Taifa kutumia mwanya huo kuvuruga amani iliyopo.

Magufuli ametoa msimamo huo leo Jumapili Septemba 15,2019 katika hotuba yake iliyosomwa na  Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii,  Jinsia,  Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu wakati wa maadhimisho ya Jubilee ya miaka 25 ya uaskofu wa Mhashamu Anthony Banzi wa Jimbo Katoliki la Tanga.

Mwalimu amesema Serikali itahakikisha inaunga mkono viongozi wa madhehebu ya dini kwa kuwa wanaaminiwa na kusikilizwa na jamii kuliko viongozi wengine.

Amefafanua mbali ya kutekeleza jukumu la kuwalea kiroho wananchi lakini pia viongozi wa dini kupitia madhehebu yao wamekuwa wakiendesha shughuli za kimaendeleo katika sekta ya afya na elimu.

Akitoa salamu za Jimbo Katoliki la Tanga, Katibu Mkuu, Padre Paul Seming'indo amesema  Askofu Banzi aliyezaliwa Oktoba 28, 1946 amekuwa mtumishi wa kanisa miaka yote na mwaka 1994 alisimikwa rasmi uaskofu wa jimbo  hilo hadi sasa.

Paul amesema katika kipindi cha muda wake, Banzi ameanzisha shule za msingi 13, vyuo vya ufundi sita, shule za awali 36, radio  zahanati na vituo vya afya saba

"Katika utumishi wake Askofu Banzi amewezesha kupanda ngazi ya upadre na uaskofu wa wale aliokuwa akiwaongoza bila vikwazo wala upendeleo," amesema   Semng'indo.

Kiongozi wa kanisa Katoliki Duniani aliwakilishwa na Balozi wa Vatican nchini Tanzania, Askofu Mkuu Marek Sokzyaski ambapo viongozi wengine waliohudhuria ni Askofu mstaafu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Polycarp Kardinali Pengo, Rais mstaafu wa awamu ya tatuwa Tanzania, Benjamin Mkapa na mkewe Anna Mkapa pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Martine Shigela