Masanja Mkandamizaji ajitosa kumrithi Filikunjombe

Msanii wa vichekesho na muimbaji wa nyimbo za injili, Emmanuel Mgaya maarufu kwa jina la ‘Masanja Mkandamizaji’.

Muktasari:

Uchaguzi wa kumpata mbunge wa jimbo hilo ulilazimika kuahirishwa baada ya kutokea kifo cha aliyekuwa mbunge na mgombea wa jimbo hilo kupitia CCM, Deogratius Filikunjombe.

Dar es Salaam. Wagombea tisa wakiwemo mdogo wa marehemu Deo Filikunjombe na mchekeshaji Masanja Mkandamizaji wamejitosa kuwania ubunge wa jimbo la Ludewa, mkoani Njombe kupitia tiketi ya Chama cha Mapinduzi (CCM).

Uchaguzi wa kumpata mbunge wa jimbo hilo ulilazimika kuahirishwa baada ya kutokea kifo cha aliyekuwa mbunge na mgombea wa jimbo hilo kupitia CCM, Deogratius Filikunjombe.

Miongoni mwa waliojitokeza kwenye kinyang’anyiro hicho ndani ya CCM ni mdogo wa marehemu, Philipo Filikunjombe na msanii wa vichekesho na muimbaji wa nyimbo za injili, Emmanuel Mgaya maarufu kwa jina la ‘Masanja Mkandamizaji’.

Filikunjombe alifariki dunia Oktoba 15, siku kumi kabla ya kufanyika Uchaguzi mkuu, kufuatia ajali mbaya ya helikopta iliyotokea katika hifadhi ya wanyama ya Selous, eneo la Kilombero, mkoani Morogoro.

Mbali na Filikunjombe, wengine waliofariki kwenye ajali hiyo ni rubani wa helkopta hiyo William Slaa, Blanka Haule na Egdi Nkwela.

Akizungumza na Mwananchi Digital, Katibu wa CCM wilaya ya Ludewa, Luciano Mbosa aliwataja wagombea wengine Johnson Mgimba, James Mgaya, Zephania Jwahula, Deo Ngalawa, Dk Evaristo Mtitu na Simon Ngatunga.

Alisema tayari wagombea hao wamechukua fomu za chama hicho ili wapate nafasi ya kuchujwa kwenye kura za maoni na kupatikana mgombea mmoja atakayeteuliwa kupeperusha bendera ya chama hicho.

“Wapo wagombea waliorejesha fomu zao na wengine natarajia kupokea leo ili tuandae terehe ya kura za maoni zitakazowachuja na kupatikana mgombea mmoja atakiwakilisha chama chetu kwenye uchaguzi wa jimbo,” alisema.

Mbosa amewataka wagombea hao kufuata sheria za uchaguzi za chama hicho kwa kufanya siasa za kistaarabu ili kuepuka makundi na migooro isiyo ya lazima.