Mchungaji mwingine Kenya akamatwa kwa tuhuma za mauaji ya waumini
Mchungaji Ezekiel Odera wa Kanisa la ‘New Prayer Centre’ akiwa ameshikiliwa na polisi kwa tuhuma za mauaji ya waumini wake
Nairobi. Polisi nchini Kenya katika Kaunti ya Kilifi wamemkamata mchungaji mwingine anayejulikana kwa jina la Ezekiel Odero kwa tuhuma za kuhusika na vifo vya waumini katika Kanisa lake linalojulikana New Prayer Centre.
Tukio hilo limetokea katika Kaunti ya Kilifi siku chache tangu kuibuliwa mauaji ya waumini wa kanisa linaloongozwa na Mchungaji Paul Mackenzie ambaye kwa sasa anashikiliwa na polisi.
Kamanda wa Polisi Kanda ya Pwani, Rhoda Onyancha amenukuliwa akisema, “Tumemkamata Mchungaji Ezekiel wa Kanisa la ‘New Prayer Centre’ kwa tuhuma za kuhusika na vifo ambavyo vimekuwa vinatokea katika eneo lake.
Waziri wa Mambo ya Ndani wa nchi hiyo, Kithure Kindiki amesema Odero anashikiliwa kwa mashtaka ya mauaji ya wafuasi wake na anaendelea kuhojiwa.
Aidha, Onyancha amesema kwa sasa wamechukua hatua ya kufunga kituo chake cha maombi na watatoa taarifa zaidi siku zijazo.