Meya Raibu awafutia faini madereva bajaji Moshi
Meya wa Manispaa ya Moshi Juma Raibu akizungumza katika mkutano na madereva bajaji Mjini humo. Picha na Janeth Joseph
Muktasari:
- Meya wa manispaa ya Moshi, Juma Raibu amewaondolea madereva bajaji wa manispaa hiyo faini ya Sh50,000 ya maegesho waliyokuwa wakidaiwa baada ya kuchelewa kulipa fedha ya maegesho ambayo ni Sh20,000 kwa mwaka.
Moshi. Meya wa manispaa ya Moshi, Juma Raibu amewaondolea madereva bajaji wa manispaa hiyo faini ya Sh50,000 ya maegesho waliyokuwa wakidaiwa baada ya kuchelewa kulipa fedha ya maegesho ambayo ni Sh20,000 kwa mwaka.
Raibu ametangaza kuondoa faini hiyo kwa siku 14 leo Jumatano Juni 2, 2021 na kuwataka madereva wa bajaji kulipa Sh20,000 na kwamba baada ya siku hizo kupita ambao watakuwa hawajalipa, watapaswa kulipa kiasi hicho pamoja na faini.
Kwa mwaka madereva bajaji hutakiwa kulipa Sh20,000 na mwisho wa kulipa ilikuwa Aprili, 2021.
Aliondoa faini hiyo baada ya kukutana na madereva hao, “vijana fanyeni kazi kwa mujibu wa sheria na taratibu zilizowekwa, nitumie fursa hii kwa niaba ya kamati ya fedha na uongozi manispaa ya Moshi, fedha zote mlizokuwa mkidaiwa nimewafutia.”
"Nimetoa kama ofa na ndani ya siku 14 muwe mmelipa fedha hiyo ambayo ni Sh20,000 ili kuepuka kudaiwa tena faini maana baada ya siku hizo watakaokuwa hawajalipa watalazimika kulipa na faini.”