Mgogoro NCCR-Mageuzi: Selasini aikingia kifua Mahakama

Makamu Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, Joseph Selasini wakati akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma leo Jumatatu Septemba 26, 2022 . Pcha na Merciful Munuo

Muktasari:

  • Makamu Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi-Bara, Joseph Selasini amewataka viongozi wa vyama vya siasa kuanza kuheshimu Katiba na demokrasia ndani ya vyama vyao kabla ya kulilia demokrasia ya nchi.

Dodoma. Makamu Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi-Bara, Joseph Selasini amewataka viongozi wa vyama vya siasa kuanza kuheshimu katiba na demokrasia ndani ya vyama vyao kabla ya kulilia demokrasia ya nchi.

Selasini ameyasema hayo leo Jumatatu, Septemba 26, 2022 jijini Dodoma wakati akimjibu aliyekuwa mwenyekiti wa chama hicho James Mbatia.

Juzi, Mbatia alisema kikao kilichofanyika mwishoni mwa wiki cha kumvua uanachama ni kuingilia uhuru wa Mahakama kwa madai uamuzi huo umefanyika kipindi ambacho kina kesi inayoendelea mahakamani.

“Mahakama ya nchi yetu imefanya kazi vizuri, isichafuliwe na watu ambao wanatafuta madaraka, isichafuliwe na waroho wa madaraka. Katika amri zote mbili hakuna iliyozuia mikutano yetu,” amesema.

Amesema viongozi wa vyama vya upinzani wanakuwa na msuli wa kuzungumzia mafisadi ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Serikali lakini wanakosa misuli ya kuzungumzia mafisadi ndani ya vyama vyao.