Mjamzito auawa baada ya kukataa kwenda kwa mganga wa kienyeji

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Songwe, Janeth Magomi

Muktasari:

Jeshi la Polisi mkoani Songwe linamshikilia mkazi wa kata ya Mlale wilayani Ileje, Shukrani Kamwela (16) kwa tuhuma za mauaji ya Subira Kibona (16).

Songwe: Jeshi la Polisi mkoani Songwe linamshikilia mkazi wa kata ya Mlale wilayani Ileje, Shukrani Kamwela (16) kwa tuhuma za mauaji ya Subira Kibona (16).

Kamada wa Polisi mkoani humo, Janeth Magomi amesema kuwa kijana Shukrani anadaiwa kumuua Subira ambaye walikuwa wanaishi pamoja kama ‘mke na mume’ kwa kumchoma na kitu chanye ncha kali.

Kamanda Magomi amesema Jeshi lilo lilipokea taarifa za kupotea kwa Subira tangu Januari 13 mwaka huu na kuanza kufuatilia.

Amesema baada ya Subira kutoonekana tangu Januari 13 wananchi walifanya juhudi za kumtafuta na kukuta mwili wake katika moja la pori ukiwa umechomwa na kitu chenye ncha kali mgongoni na kuchomwa moto huku ukiwa umetupwa kwenye korongo.

Kamanda Magomi amesema kuwa mwili wa msichana huyo ulipatikana Jumapili Januari 16, 2022.

Inadaiwa kuwa kijana huyo alimuambia marehemu ambaye alikuwa mjamzito kuwa waende kwa mganga wa kienyenji kutafuta dawa ya tumbo maarufu kama kata Kamba.

Dawa hiyo inadaiwa kuwa inasaidia mtu kujifungua salama kwani marehemu alikuwa na ujauzito wa miezi saba lakini marehemu alikataa kwenda kwa mganga huyo.