Mvua yaacha kaya 50 bila makazi Wilaya ya Mtwara
Muktasari:
Mkuu wa Wilaya ya Mtwara, Dunstan Kyobya amesema wakazi wanaoishi karibu na bwawa wameathirika sana
Mtwara. Zaidi ya kaya 50 za Kata ya Ziwani Halmashauri ya Wilaya ya Mtwara zimekosa makazi baada ya nyumba zao kubomoka na kujaa maji kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha.
Akizungumzia madhara hayo, Ofisa Mtendaji wa Kata ya Ziwani, Abdallah Makombo amesema baada ya mvua kubwa kunyesha na kusababisha bwawa kujaa, imesababisha maji hayo kuvuka na kuingia kwenye makazi ya watu na kuathiri zaidi Kijiji Cha Msakala.
Amesema nyumba tatu zimebomoka huku nyumba 48 zikiwa zimezingirwa na maji.
"Mvua iliyonyesha kubwa , ndio maana hata madhara yalikuwa makubwa hata barabara ilikuwa haipitiki, Tanroads( Wakala wa Barabara Tanzania) ilitusaidia kwa kutuwekea mitaro iliyosababisha maji kupungua," amesema Makombo.
Mkuu wa Wilaya ya Mtwara, Dunstan Kyobya amesema wakazi wanaoishi karibu na bwawa wameathirika sana, hivyo ni muhimu wahame.
"Namuagiza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mtwara Erica Yegella na wataalamu wake waangalie namna ya kutumia bwawa hilo ili liwe na manufaa kwa wananchi wakati, " amesema Kyobya.