Mwanamke abakwa na kuuawa Masasi

Muktasari:

Jeshi la Polisi mkoani Mtwara linawatafuta watu waliohusika kumbaka na kumuua mkazi wa Wilaya ya Masasi, Gloria Degimi Luoga (22) na kisha kuutupa mwili wake kichakani.


Mtwara. Jeshi la Polisi mkoani Mtwara linawatafuta watu waliohusika kumbaka na kumuua mkazi wa Wilaya ya Masasi, Gloria Degimi Luoga (22) na kisha kuutupa mwili wake kichakani.

Akizungumza na waandishi wa habari jana Ijumaa Desemba 2, Kaimu Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mtwara, ACP Nicodemus Katembo amesema kuwa uchunguzi wa tukio hilo unaendelea, ambapo taarifa za awali zinaonyesha kuwa mwili wa mwanamke huyo ulipatikana Desemba Mosi.

Katembo amesema kuwa baada ya uchunguzi wa kitabibu, madaktari wamebaini kuwa kifo cha mwanamke huyo kimesababishwa na kukosa hewa baada ya kuzibwa pua na mdomo na kabla ya kuuawa marehemu alibakwa.

“Jeshi la Polisi Mkoa wa Mtwara linafanya juhudi kuelimisha jamii kupitia dawati la jinsia pamoja na wakaguzi wa kata kuhusu ukatili wa jinsia.

“Natoa rai kwa jamii kuunga mkono juhudi hizo ili kuhakikiksha kuwa vitendo hivyo vya kihalifu vinavyoweza kugharimu maisha ya watu vinakomeshwa,” amesema Katembo