Mwanamke atoka akichekelea kwa Makonda

Muktasari:

Ameiambia MCL Digital kuwa mwanamume  amekubali kuhudumia watoto wake, jambo ambalo amekuwa akilikataa kwa muda mrefu.


Dar es Salaam. Wakati baadhi ya wabunge na mawaziri  wakiendelea kuhoji uhalali wa kampeni ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, mwanamke mmoja, Mary Masawe ameondoka kwenye ofisi za mkuu huyo wa mkoa akichekelea.

Mary ambaye anadai kutelekezwa kwa miaka tisa na mwenza wake aliyezaa naye watoto wawili ni miongoni mwa wanawake waliopata msaada wa kisheria.

Ameiambia MCL Digital kuwa mwanamume huyo amekubali kuhudumia watoto wake, jambo ambalo amekuwa akilikataa kwa muda mrefu.

Amesema mara kadhaa alikuwa akimpeleka kwenye vyombo vya sheria lakini alikuwa mgumu kuitikia wito.

"Sijui hata nifanyeje miaka mingi amekataa kuwahudumia watoto wake, nampelekea barua za wito anajibu hana muda,lakini hii ya Makonda kiboko mwenyewe amekuja," amesema.