Ndalichako awataka waongoza watalii nchini kuwa mabalozi

Arusha. Waziri wa Kazi, Ajira, Vijana na wenye ulemavu, Profesa Joyce Ndalichako  amewataka waongoza watalii nchini kuwa mabalozi wazuri katika kutangaza vivutio vya utalii sambamba na kuwapeleka watalii kujionea  vivutio hivyo ili kuweza kufurahia neema ya kipekee iliyopo katika nchi yetu.

Hayo yamesemwa leo Juni 17, 2023 jijini Arusha wakati akifunga mafunzo ya kukuza ujuzi kwa waongoza watalii yaliyoandaliwa na Ofisi ya Waziri Mkuu kazi, Ajira, Vijana na wenye ulemavu kwa kushirikiana na TTGA  yaliyofanyika kwa muda wa siku sita jijini hapa.

Ndalichako amesema ni jukumu la waongoza watalii kuhakikisha wanatangaza vivutio hivyo kwa wageni mbalimbali wanaofika nchini ili kuongeza idadi ya watalii watakaotembelea vivutio  hivyo kwa wingi na hatimaye kuongeza pato la Taifa.

Aidha amewataka kutoa huduma nzuri kwa watalii hao na kuwa wakarimu pamoja na kutumia lugha nzuri ili sekta ya utalii iendelee kukua zaidi na kuwashawishi watalii kuendelea kutembelea kwa wingi vivutio vyetu.

Aidha amewataka waajiri nchini kuhakikisha wanatii  sheria za kazi bila shuruti  ikiwemo kulipa mishahara ya wafanyakazi wao kwa wakati kwani serikali  ina dhamira  ya dhati kuhakikisha wafanyakazi wanafanya kazi kwa weledi.

"Utekelezaji wa mafunzo haya ya kukuza ujuzi kwa wafanyakazi ni muhimu sana na yatakuwa endelevu kwani ni lazima muwe  na ujuzi stahiki wa kuongoza watalii vizuri kwani nyie ndio mnaokuwa  na wageni hao muda mwingi na hivyo mna kila sababu ya kutumia  ujuzi wenu ipasavyo kuhakikisha mnawaridhisha watalii  hao," amesema Profesa Ndalichako

Kwa upande wake Mtendaji Mkuu wa TPSF, Raphael Maganga amesema kuwa utoaji mafunzo hayo kwa waongoza watalii hao utasaidia sana kuwa mabalozi wazuri katika utendaji kazi wao na kuongeza idadi ya watalii na kuweza kufikia malengo yaliyowekwa .

Maganga amesema sekta  ya utalii inaendelea kukua sana na inaendelea kuajiri zaidi ya Watanzania milioni 1.5 ikiwa ni sekta inayoajiri watanzania wengi sana.

"Taasisi ya sekta binafsi Tanzania (TPSF) tunaendelea kushirikiana na serikali  katika kuhakikisha makampuni  ambayo hayatoi mikataba yanafuatiliwa ili watu waweze kupata haki zao za msingi," amesema

Mwenyekiti wa Chama cha Waongoza Watalii Tanzania (TTGA), Lembris Loipuko  amesema jumla ya waongoza watalii 696 kutoka kanda ya kaskazini wameweza kupata mafunzo hayo ambapo  mada mbalimbali zimetolewa ikiwemo huduma kwa wateja, huduma ya kwanza ya kisasa, utangulizi wa huduma ya uongozi wa watalii wandani .

Amesema kupitia mafunzo hayo wataweza kuyafanyia  kazi yale yote waliyojifunza ili kuunga juhudi za Rais Samia Suluhu Hassan ya kukuza utalii nchini pamoja na juhudi za serikali za kufikia watalii milioni 5 ifikapo mwaka 2025.

Aidha amesema pamoja na mafanikio mbalimbali, wameomba serikali iwasaidie kuwa na vifurushi  rafiki kwa waongoza watalii kwani wanasikitishwa sana na serikali kusitisha huduma na kukataa kuhuisha vifurushi vya Bima ya Afya kupitia NHIF ambavyo waongoza watalii walikuwa wanufaika.

Aidha waliomba serikali kuwapatia gari la kutoa msaada kwani kwa upande wa Mlima Kilimanjaro halipatikani kwa wakati jambo linalopelekea kuhatarisha maisha ya wageni na wapanda mlima kwa ujumla.