Ngoma bado ngumu Kariakoo

Mwenyekiti wa wafanyabiashara Kariakoo, Martin Mbwana akiwatuliza wafanyabiashara ambao wamegoma kuendelea na biashara. Picha na Aurea Simtowe

Muktasari:

  • Wafanyabishara Kariakoo wakubaliana kufunga maduka hadi ijumaa au Rais Samia Suluhu Hassan atakapotokea kuwasilikiza na wakiwaonya atakayefungua atakiona cha moto.

Dar es Salaam. Licha ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Amos Makalla kumaliza mgomo wa wafanyabiashara na kuwataka warejee katika biashara zao,  ngoma bado ngumu kwa Mwenyekiti wa soko hilo baada ya wafanyabiashara kugoma kufungua biashara.

Hiyo ni kutokana na kile walichoeleza kuwa wako tayari kufunga maduka hadi jioni kama hawatasikilizwa huku wakimtaka Rais kuwasikiliza.

Wafanyabiashara wa Kariakaoo leo Jumatatu Mei 15, 2023 wamegoma kufungua maduka yao kwa ajili ya kushinikiza Serikali kuingilia kati utitiri wa kodi wanaotozwa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).

Msimamo huo walianza kuuonyesha tangu Makalla akizungumza kwani katika baadhi ya vitu alivyosema wafanyabiashara walikuwa wakitoa sauti za kugomea kile anachokizungumza hasa aliposema kuwa Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa atafanya kikao na kamati ya wafanyabiashara wa soko hilo siku ya Alhamisi Dodoma.

Wafanyabiashara walisema hawaoni sababu ya wao kumfuata Waziri Mkuu Dodoma badala ya wao kufuatwa Kariakoo.

Licha ya kuonyesha kukubali lakini wafanyabiashara walibaki katika eneo hilo jambo lililomfanya mwenyekiti kuanza kuzungumza nao huku akiwasisitiza warejee katika biashara zao.

Mmoja wa wafanyabiadhara ambaye hakutaja jina lake alipopewa nafasi ya kuzungumza ikiwa wanataka kurejea katika biashara alisema lengo lao lilikuwa kukutana na Rais Samia Suluhu Hassan na si Mkuu wa Mkoa.

"Hawa wote waliokuja tumeshawasikiliza, Waziri wa Fedha ameshatusikiliza na hakuna kilichofanyika," alisema mfanyabiashara huyo huku akishangiliwa na wafanyabiashara wenzake.

Honest Kalisti Mjunbe wa Jumuiya ya wafanyabiashara amesema hakuna kurudi nyuma katika hili waliloanzisha

"Mambo ya siasa kwenye biashara zetu hatuhitaji siasa hazina nafasi, Waziri mkuu si kama hajui, Mwigulu Nchemba si Kama hajui, Mkuu wa Mkoa na Wilaya wanajua lakini hakuna kilichofanyika,"amesema.

"Cha msingi waende wakae kwenye kamati yao sisi maduka tunafunga ili tuonane na Rais Samia Suluhu Hassan,”ameongeza.