Panya wavamia mashamba na kufanya uharibifu

Flozina Manjavila mkulima Nanyumbu akiwa ameshika panya waharibifu mashambani.

Muktasari:

  • Zaidi ya ekari 2447 za mashamba ya mazao mbalimbali wilayani Nanyumbu zimeshambuliwa na panya.


Nanyumbu. Zaidi ya ekari 2447 za mashamba ya mazao mbalimbali wilayani Nanyumbu zimeshambuliwa na panya.

Akizungumza na Mwananchi Afisa Kilimo wa Kata ya Mikangaura, Dorice Ashapila amesema katika kata hiyo vipo vijiji sita ambapo vyote vimeripoti kuathiriwa na panya katika mashamba yake.

“Wakulima wetu huwa wanapalilia mapema kabla ya mvua kunyesha walipokuja kufanya palizi walikuta uharibifu mkubwa shambani uliofanywa na panya ambapo wamefikia hatua ya kuchukua vyakula walivyotunza na kufanya mbegu kwakuwa kila wanapopanda mazao yanaathiriwa”

Nae Jabir Murio mkulima na mkazi wa kijiji cha Kilosa wilayani humo amesema mashamba mengi yamejaa mashimo ya panya ambao wamkuwa wakichimba na kung’oa mazao kwa zaidi ya awamu nne hali ambayo inawafanya wakulima kupata hofu na kuomba msaada kwa serikali.

“Haya mashimo unayoayaona ni ya panya wamekuwa wasumbufu kwa kiasi kikubwa tumelazimika kuwachimbia mashimo ili kuwatoa wanatusumbua wameharibu mashamba yetu kwa kiasi kikubwa zaidi ya heka sita.

“Serikali isikilize kilio chetu, mvua zimechelewa na panya wanatuathiri sana hatuna biashara zaidi ya kili mo, ukiangalia wanakata mazao yote hata mbegu tumeishiwa, yaani tukipanda tena ni mpando wa nne”

Naye Flozina Manjavila amesema kuwa kwa wanaomba msaada wa haraka ili kuwadhibiti panya hao kabla mvua hazijaisha.

“Shamba langu lina ekari tatu nimepanda mahindi zaidi ya mara nne yote yanafukuliwa na panya na mengine yanayoota wanayavunja hata ukiangalia shamba langu lina mashimo wakati mwingine nawachimba na kuwaua ili kunurusu mimea shambani”

 Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya Nanyumbu, Mashaka Mfaume alikiri kuwepo tatizo hilo ambapo amesema kuwa Wilaya hiyo ina vijiji 94 ambapo asilimia 90 ya wakazi ni wakulima.  

“Kwakweli hili tatizo ni kubwa na tumeona  mazao yanashambuliwa na panya  yaani zaidi ya  hekta 1470 zimesharipotiwa kushambuliwa na panya.Hili kwetu limekuwa tatizo kubwa ndio maana tumeomba Wizara  ya Kilimo ituletee sumu ili tuweza kuwadhibiti tusipo wadhibiti athari zake ni kubwa” amesema Mfaume