Polisi wazungumzia msako anayedaiwa kumuua mama na mwanaye

Siri ya mama na mwanaye waliofia gesti Moshi

Muktasari:

  • Polisi mkoani Kilimanjaro wanaendelea kumsaka mtuhumiwa wa mauaji ya Irene Lyimo na mwanaye wa miaka miwili ambao miili yao ilikutwa katika nyumba ya  kulala wageni kata ya Marangu Magharibi Wilaya ya Moshi mkoani humo.

Moshi. Polisi mkoani Kilimanjaro wanaendelea kumsaka mtuhumiwa wa mauaji ya Irene Lyimo na mwanaye wa miaka miwili ambao miili yao ilikutwa katika nyumba ya  kulala wageni kata ya Marangu Magharibi Wilaya ya Moshi mkoani humo.

Akizungumza na Mwananchi Digital leo Ijumaa Mei 5, 2021 kaimu kamanda wa polisi mkoani humo, Ronald Makona amesema  jitihada za kumtafuta mtuhumiwa wa mauaji hayo  zinaendelea.

Machi 2, 2021,  Makona alisema mwili wa mwanamke huyo na mwanaye ilikutwa katika nyumba hiyo ya kulala wageni ikiwa imeharibika na kwamba kabla ya umauti kumfika, mwanamke huyo alionekana akiingia kwenye nyumba hiyo na mwanaume mmoja anayedaiwa kutoweka kusikojulikana.

Kwa mujibu wa diwani wa kata hiyo, Filbert Shayo kwenye kitabu cha wageni ilionekana watu watatu wameingia katika nyumba hiyo Februari 23, 2021 na miili ilikutwa Machi 2.