Rais Mwinyi ameeleza nia ya kuanzisha Mahakama ya Rushwa na Uhujumu uchumi

Rais Mwinyi ameeleza nia ya kuanzisha Mahakama ya Rushwa na Uhujumu uchumi

Muktasari:

  • Rais  wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk Hussein Mwinyi  amesisitiza mkakati wa kuanzisha Mahakama ya rushwa na uhujumu wa uchumi visiwani humo. 

Rais  wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk Hussein Mwinyi  amesisitiza mkakati wa kuanzisha Mahakama ya rushwa na uhujumu wa uchumi visiwani humo. 
Taarifa iliyotolewa na Ikulu ya Zanzibar imesema Rais Mwinyi ameyasema leo Februari 8 katika maadhimisho ya 10 ya Siku ya Sheria Zanzibar, hafla iliyofanyika katika ukumbi ya Sheikh Idrissa Abdulwakil, Kikwajuni jijini Zanzibar yaliyohudhuriwa na viongozi mbalimbali walihudhuria kutoka Zanzibar na Tanzania Bara.
“Rais Mwinyi ameitaka Mahakama ijipange kwa lengo la kuanzisha kwa Mahakama hiyo kutokana na umuhimu wake mkubwa hapa Zanzibar,” imesema taarifa hiyo. 
Imesema pia, Rais Dk Mwinyi ameeleza kufurahishwa kwake na kutekelezwa kwa maelekezo ya kuanzishwa kwa Mahakama  maalum ya udhalilishaji itakayosaidia kuharakisha kusikilizwa na kutolewa maamuzi kwa kesi za aina hiyo. 
“Rais Mwinyi amesema kuwa  ni vyema mahakama ikaimarisha juhudi za kutoa elimu ya sheria kwa kuzingatia mahitaji ya kiuchumi na kijamii pamoja na mabadiliko ya sayansi na teknolojia.”