Rais Samia amteua Tutuba Gavana mpya BOT

Emmanuel Tutuba kabla ya kuteuliwa kuwa Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BOT). Picha na mtandao.

Muktasari:

  • Rais Samia Suluhu Hassan amefanya uteuzi wa viongozi ambapo amemteua  Emmanuel Mpawe Tutuba katibu mkuu wizara ya fedha na mipango kuwa Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT).

Dar es Salaam. Rais Samia Suluhu Hassan amemteua Emmanuel Tutuba aliyekuwa katibu mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango kuwa Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BOT).

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo Januari 7, 2022 na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais Ikulu, Zuhura Yunus, Tutuba amechukua nafasi ya Profesa Luoga ambaye muda wake umekwisha.

Taarifa hiyo inaeleza kwamba  Rais Samia amemteua pia Dk Natu Mwamba kuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango akichukua nafasi ya Tutuba.

"Dk Mwamba alikuwa mhadhiri mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na mwenyekiti wa bodi ya kampuni ya uendeshaji wa kiwanja cha ndege cha Kilimanjaro (Kadco)," inaeleza taarifa hiyo.

Taarifa hiyo ya Ikulu inaeleza kwamba uteuzi huo unaanza mara moja.

Profesa Luoga aliteuliwa na Rais wa awamu ya tano, Hayati John Magufuli, Oktoba 23, 2017 akichukua nafasi ya  Benno Ndulu ambaye alistaafu kama Gavana wa BOT.

Profesa Luoga ambaye alitolewa katika chuo Kikuu Cha Dar es Salaam, ametumikia wadhifa huo kwa muda wa miaka mitano huku akikumbana na changamoto za kuongezeka kwa deni la taifa na mdororo wa uchumi uliosababishwa na mlipuko wa ugonjwa wa Uviko-19 na vita vya Ukraine na Russia.