Rais Samia: Sijaridhishwa na kasi ya UWT

Rais wa Tanzania na Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Samia Suluhu Hassan akizungumza na viongozi, wageni mbalimbali pamoja wajumbe wa Jumuiya ya Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) kabla ya kufungua Mkutano wa 10 wa Jumuiya hiyo unaofanyika kwenye ukumbi wa Mikutano wa Jakaya Kikwete Jijini Dodoma Novemba 28, 2022.

Muktasari:

Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rais Samia Suluhu Hassan ameeleza kutoridhishwa na kasi ya kujiunga kwa wanachama wa Jumuiya ya wanawake wa chama hicho (UWT) na uendeshaji wa miradi yake ya kiuchumi.

Dodoma. Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rais Samia Suluhu Hassan ameeleza kutoridhishwa na kasi ya kujiunga kwa wanachama wa Jumuiya ya wanawake wa chama hicho (UWT) na uendeshaji wa miradi yake ya kiuchumi.

  

Rais Samia ameyasema hayo leo Jumatatu Novemba 28, 2022 wakati akizungumza kwenye mkutano mkuu wa uchanguzi wa UWT jijini Dodoma.


Samia amesema kuanzia mwaka 2017 hadi 2022 Jumuiya hiyo imeingiza wanachama wapya 86,288 ambao amesema sio idadi nzuri kwao.


“Ukichukua idadi hiyo ukiigawa kwa mikoa 32 na kujua mikoa mengine ni midogo sana kama ile ya Zanzibar unapata wanachama 2697 tu sasa hii sio kazi nzuri sana,” amesema.


Samia amesema jumuiya hiyo ilikuwa na muda wa kutosha wa kuongeza wanachama wengi zaidi wakati nchi ilipokuwa haina hekaheka za kisiasa na kutumia makongamano kujitangaza.


Akizungumzia upande wa miradi ya kiuchumi, Rais Samia amesema miradi hiyo haijaipa UWT nguvu kubwa ya kiuchumi hivyo kuwa na tabia ya kushika na kuacha miradi hiyo.

Amesema miradi inayoendeshwa na Jumuiya hiyo mingi ni ya vibanda, mashine za kusaga na mingine midogo ambayo haijaipa nguvu kiuchumi UWT.

“Wito wangu kwa Jumuiya ni kwenda kufanya miradi mikubwa itakayoipa Jumuiya nguvu ya kiuchumi,” amesema Samia.


Rais Samia amesema aliona wakati wa maandalizi ya kuingia kwenye mchakato wa uchaguzi huo namna Kamati mbalimbali zilifatwa kuangalia upatikanaji wa fedha.

“Baadae nikasema msisumbuke kwa hiyo chama na mimi tukatoa fedha mambo yakaenda, hii inaonesha kuwa miradi tuliyonayo bado haijawa miradi ya kutupa nguvu ya kiuchumi kwenye Jumuiya,” amesema Samia.

Pamoja na mambo mengine, mkutano huo utafanya uchaguzi wa viongozi mbalimbali wakiwemo wa nafasi ya uenyekiti ambapo wagombea watano wanachuana vikali.

Wagombea waliopitishwa na Halmashauri Kuu ni, Gaudentia Kabaka (anayetetea nafasi yake), Kate Kamba, Dk Wemael Chamshama, Mariam Lulinda na Mary Chatanda huku mchuano mkali ukionekana kwa Gaudentia Kabaka, Kamba na Mary Chatanda.