Rais Samia: Tutafanya mabadiliko kwenye elimu, polisi

🔴#Exclusive: Mahojiano maalumu na Rais Samia Suluhu Hassan

Muktasari:

  • Rais Samia Suluhu Hassan amesema mapendekezo yaliyotolewa na tume zilizoundwa kuchunguza matukio yaliyofanywa na baadhi ya askari polisi baada ya malalamiko ya wananchi yataleta “mabadiliko kidogo ndani ya jeshi hilo”.


Dodoma. Rais Samia Suluhu Hassan amesema mapendekezo yaliyotolewa na tume zilizoundwa kuchunguza matukio yaliyofanywa na baadhi ya askari polisi baada ya malalamiko ya wananchi yataleta “mabadiliko kidogo ndani ya jeshi hilo”.

Rais Samia alibainisha hayo wakati wa mahojiano aliyofanya na vyombo vya habari vya Kampuni ya Mwananchi Communications Ltd (MCL) - magazeti ya Mwananchi, The Citizen, Mwanaspoti na Mwananchi Digital yaliyoongozwa na Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni hiyo, Bakari Machumu.

Akijibu swali la mikakati ya Serikali itakayofanya raia wawe na imani na Jeshi la Polisi, Rais Samia alisema licha ya CCM kuwaelekeza kuchukua hatua, pia kuna mapendekezo yaliyotolewa na tume zilizoundwa kuchunguza matukio ya polisi yatakayofanyiwa kazi.

Mbali na suala hilo, pia Rais alizungumzia mabadiliko makubwa yatakayofanyika katika mfumo wa elimu ili kuhakikisha ujuzi unaopatikana unamsaidia mhitimu katika nyanja za maisha kuliko hali ilivyo sasa.

Swali: Chama cha Mapinduzi (CCM) kimeielekeza Serikali yako kuhusu malalamiko dhidi ya polisi, Serikali ina mkakati gani kuona kwamba raia wanakuwa na imani jeshi hilo?

Jibu: Chama kimetuelekeza kama mlivyosikia na yanayotokea sisi wenyewe kama Serikali tuliunda tume kadhaa kwenda kuangalia, yale yaliyotokea hivi karibuni na hayo mengine, tayari tumepata ripoti ya zile tume tulizounda.

Wamekuja na mapendekezo kadhaa, kwa hiyo tunakwenda kutekeleza hayo mapendekezo na tutakapotekeleza, basi mtasikia kwamba kuna hili limetekelezwa.

Ni mapendekezo ambayo yataleta mabadiliko kidogo ndani ya Jeshi la Polisi.

Swali: Uongozi wako unataka kuacha alama gani katika kuwawezesha wanawake?

Jibu: Wanawake ni elimu, wanawake ni afya, wanawake ni maji, wanawake ni uchumi. Kuwawezesha kiuchumi. Tunapozungumzia kuwawezesha wanawake, watu wengi wanakwenda tu kiuchumi. Kwanza lazima umjenge afya yake iwe nzuri, umpe elimu ya huo uchumi anaokwenda kuujenga, aelewe anakwenda kufanya nini. Kwa hiyo ni elimu na ujuzi.

Ili umjengee maarifa ya kile anachokwenda kukitekeleza, lakini umesema hapa kwamba maendeleo yanaletwa na vitu vinne -- siasa safi, uongozi bora, watu. Lakini kwenye falsafa nyingine inasema maendeleo ni mtaji, ardhi na nguvu kazi. Nguvu kazi ni wanawake wenyewe lakini lazima tuwawezeshe, wawe na maeneo ya kufanyia kazi, lazima tuwawezeshe wawe na mitaji na hizo ndizo hatua tunazochukua kupitia mabenki na taasisi mbalimbali za fedha kwenda kuwawezesha wanawake.


Mapinduzi ya elimu

Swali: Katika suala la elimu Watanzania watarajie mapinduzi ya namna gani, hasa kwa vijana na Watanzania kwa ujumla ili waweze kuwa na uelewa na wapate fursa ya kushiriki kwenye uchumi.

Jibu: Kwenye elimu, ni kweli sasa hivi tunaangalia kufanya mageuzi kwenye mfumo wetu wa elimu kwa sababu mie nikikaa na watu wa sekta ya elimu siku zote huwa narudia msemo wa yule mbunge Kishimba (Jumanne Kishimba mbunge wa Kahama Mjini), anasema, kwani aliwaambia nyinyi Serikali, ‘kwamba mtoto lazima aende darasa la kwanza, la pili, la tatu, la nne, la tano, la sita? Kwa nini hamumtazami mtoto ana mwelekeo gani mkamuelekeza huko, akatoka mapema akaenda kwenye field ambayo anaweza akaifanyia kazi?’

Lakini anasema pia kwamba ‘mnachukua mtoto (wake), mnampitisha madarasa yote, mnamchukua akiwa na miaka sita, saba mnanirudishia akiwa na miaka 23, 24 na 27 anarudi na cheti tu kinaitwa digrii, hajui kulima, hajui kuchonga, hajui chochote, halafu mnaniambia ajiajiri anaanzia wapi?’

Yale maneno ukiyatazama, aliyasema bungeni, alichekesha, lakini hayakuwa ya kuchekesha kwa kweli, yalikuwa ni maneno ya kuyapa uzito.

Kwa hiyo tulichofanya ni kwamba tumekubaliana kwamba sasa tuelekee kwenye elimu ujuzi, badala ya elimu taaluma peke yake. Elimu taaluma sawa, lakini elimu ujuzi. Elimu ujuzi ni ile ambayo itampa mtoto mwelekeo anapotoka kidato cha nne na hakubahatika kwenda cha tano na cha sita, angalau anajua nielekee wapi, kuna nini na nitakwenda kufanya nini.

Na kwa hiyo, ndio maana sasa tunabadilisha mtalaa wa elimu Tanzania. Nadhani mmeshuhudia mikutano kadhaa pande zote mbili za Muungano za kutaka maoni ya wananchi kwenye mtalaa wa Tanzania, mchakato unaendelea, utakapofikia mwisho tutafanya vikao vya mwisho kushirikisha watu, tuone kwamba huu ndio mtalaa tunaokubaliana nao.

Lakini katika ule mtalaa pia la muhimu na kubwa zaidi mbali ya elimu ujuzi, mtoto wa Kitanzania anapopata elimu ajijue yeye ni Mtanzania na kuwa Mtanzania maana yake nini, Tanzania ina thamani gani kwake, kwa nini ailinde Tanzania.

Tunataka aweze kujua hayo yote. Kwa hiyo tunabadilisha mtalaa wa elimu, lakini, pili tumejielekeza sasa kwenye kuweka nguvu kwenye kile kwetu tunasema elimu amali, elimu itakayompa mtu uwezo wa kufanya kitu, huku wanasema Veta -- elimu ya ufundi stadi.

Kwa hiyo tutajielekeza sana huko, kila wilaya tunakwenda kujenga vyuo hivyo na hivyo vitakwenda kufundisha yale mambo ambayo kwenye wilaya ile labda ndio kitu kikubwa kinachofanywa ili kuwatayarisha vijana waelekee kwenye hilo.

Lakini jingine ni kwamba sasa hivi ulimwengu unakwenda na mitandao, kwa hiyo tuna matarajio ya kuweka chuo kikubwa cha shughuli za mitandao, kufundisha vijana wetu ili wasiachwe na ulimwengu.

Waende na ulimwengu pamoja na ujuzi mbalimbali watakaokuwa nao, lakini kwenye kazi zao hizohizo kwa kiasi kikubwa watatumia mitandao, kutafuta utaalamu zaidi ni mitandao, kutafuta soko zaidi ni mitandao, kujua mtaji uko wapi ni mitandao, kila kitu ni mitandao, kwa hiyo tunakwenda kuweka mkazo kwenye hilo pia.


Tanzania anayoitaka

Swali: Je, ungependa kuiona Tanzania imefika wapi ndani ya miaka mitatu ijayo kiuchumi, kijamii na kisiasa?

Jibu: Mitatu ni karibu sana, lakini niseme tu kipindi chochote kile ningependa kuona Tanzania ambayo ina Watanzania wanaojielewa kama nilivyosema mwanzo, kwamba wao ni Watanzania, utaifa wao ni wa Utanzania na wana wajibu kuitumikia Tanzania na kulinda Tanzania, kulinda mali za Tanzania.

Watanzania wa aina hiyo, Mtanzania ambaye hataambiwa ingia barabarani, piga makelele ukikuta gari ya mtu piga jiwe, ukikuta nini choma, aseme hapana.Mimi ni Mtanzania hili ni Taifa langu, nikifanya hivi natia dosari taifa langu, lakini Tanzania ambayo itakuwa na upeo mpana wa mazungumzo, panapotokea changamoto tukae, tuzungumze tujue tatizo liko wapi tunalitatua wote tuende mbele.

Tanzania ambayo hakuna mtu anakosa chakula kwa siku na yale mahitaji muhimu hakuna mtu anayakosa kwa siku. Sasa hayo hayatakuja kwa miaka mitatu yatakuja kwa miaka labda mitano, saba, kumi huko mbele kwa hiyo naweza mimi nikatoka akaja mwingine akaendeleza. Lakini, mapenzi yangu nilikuwa natamani Tanzania hiyo.

Ni kuona Tanzania inashindana na giant (mataifa makubwa) ndani ya Afrika kama Afrika Kusini, Nigeria wale giant wa kaskazini kwa Afrika, Tanzania nasi tutajwe.

Lakini ningependa kuiona Tanzania inayodumisha amani na utulivu kama tulivyo hivi. Tanzania ambayo inafanya siasa za kistaarabu, demokrasia imeshamiri na siasa zinafanywa kwa ustaarabu, hiyo ndiyo Tanzania ambayo ningependa mimi kuiona inakua kiuchumi, demokrasia inashamiri, siasa za kistaarabu, kila mtu yuko happy (ana furaha) ana amani ya moyo.

Maana kuna amani ya nchi hatupigani, lakini amani za mioyo hakuna, kwa hiyo ningependa watu wawe na amani za mioyo pia.

Swali: Nini tutarajie sasa kwamba nchi inaendesha siasa za kukubaliana kutokukubaliana, kutofautiana, lakini tukabaki tunaheshimiana.

Jibu: Kama nilivyosema tukuze demokrasia yetu Tanzania, lakini tufanye siasa za kistaarabu, halafu ajenda ya maendeleo iwe yetu sote, ajenda ya amani ya Taifa la Tanzania iwe yetu sote bila kujali itikadi zetu za siasa, bila kujali dini zetu, bila kujali makabila yetu, bila kujali yote hayo kama unaitwa Mtanzania jukumu la kuhakikisha Tanzania inabaki salama, maendeleo yanapatikana, demokrasia na siasa za kistaarabu zinafanywa Tanzania, hilo jukumu liwe letu sote. Haliwezi kuendeshwa na Serikali peke yake au chama kimoja peke yake, hapana, ni jukumu letu sote kwa sababu Tanzania ni Taifa letu sote.

Swali: Kufanyika mikutano ya vyama, hili na lile la Katiba tutarajie lini?

Jibu: Kwani uchumi umeshatengemaa? Uchumi haujatengemaa. Kwa hiyo bado tunashughulika na uchumi. Pili, nimezungumza hapa kushamirisha demokrasia. Kushamirisha demokrasia ndiyo hayo kuvipa nafasi vyama vya siasa vitumie democratic space (fursa ya kidemokrasia) yao. Wazungumze na wananchi wao, lakini nimesema hapa siasa za kistaarabu, ambao ni wajibu wetu sote.

Kwa hiyo kumzuia mtu asifanye mikutano inasaidia kwa sababu nchi itabaki na amani, hakuna vurugu, hakuna kujibishana, watu wanaelekea kwenye kitu kimoja, kuchapa kazi na kuleta maendeleo. Lakini mwingine kazi yake ni hiyo siasa, kwa hiyo ukimzuia umezuia kufanya kazi yake. Kwa hiyo na yeye ajisikie anafanya kazi yake lakini afanye akiwa anajua kwamba wote tuna ajenda ya maendeleo, kwamba Tanzania inatakiwa kuendelea na si kuharibu maendeleo.

Tuna ajenda za kulinda rasilimali zetu, si kuharibu rasilimali zetu, tuna ajenda ya kukuza demokrasia na kufanya siasa njema, si kuleta Tanzania kila siku iko kwenye BBC, kwenye CNN, Sky hapana. Au Mwananchi tena ndio chapuoo, mmepata news ya kuandika. Yaani tufanye siasa ambayo mtu akija aseme Tanzania kuna vyama vingi, lakini wametulia mpira unachezwa.

Huko zamani tulikuwa tunachochewa kule Zanzibar, hakuna kinachofanyika ni kujibishana mwanzo mwisho, tulipokaa kwenye meza ya demokrasia, tukazungumza, tukakubaliana, tukasema twende hivi, sasa hivi maendeleo juu kwa juu.

Na unaingia Baraza la Wawakilishi na hujui nani mpinzani, wote ajenda yao ni maendeleo ya wananchi wao, maendeleo ya nchi yao. Pale Serikali inapokosea kosoa waambie hapa mmekosea mngefanya hivi ingekuwa vizuri zaidi, Serikali itasikiliza watafanya.