Samia kuapishwa kuwa Rais wa Tanzania leo Ikulu Dar
Muktasari:
- Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan leo Ijumaa Machi 19, 2021 ataapishwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Dar es Salaam. Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan leo Ijumaa Machi 19, 2021 ataapishwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Kwa mujibu wa mkurugenzi msaidizi kitengo cha habari Maelezo, Rodney Thadeus hafla ya uapisho itafanyika Ikulu Dar es Salaam saa 4 asubuhi na kushuhudiwa Samia akiwa rais wa sita wa Tanzania kuchukua nafasi ya Dk John Magufuli aliyefariki dunia Machi 17, 2021.
Samia alikuwa makamu wa rais kuanzia mwaka 2015 na kuendelea na wadhifa huo baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2020.
Taarifa za kifo cha Rais Magufuli zilitangazwa jana na Samia akisema Magufuli alifariki dunia saa 12 jioni kwa maradhi ya moyo baada ya kulazwa katika hospitali ya Mzena tangu Machi 6, 2021.
Kwa mujibu wa katiba ya Tanzania rais aliyeko madarakani akifariki dunia hakuna uchaguzi mwingine unaofanyika badala yake makamu wa rais ataapishwa kuwa rais kwa kipindi kilichosalia.
Kwa mujibu wa katiba ibara ya 37 (5) baada ya Samia kuapishwa atashauriana na chama anachotoka (CCM) kisha atamteua mtu atakayekuwa makamu wa Rais.