Serikali yafuta gwaride sherehe za Uhuru

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu), George Simbachawene

Muktasari:

Tayari Wizara ya Nchi katika Ofisi ya Rais (Tamisemi) imeshabainisha mikoa itakayonufaika na fedha zilizotakiwa kugharimia gwaride la uhuru, kuwa ni pamoja na Shinyanga, Singida, Tabora, Lindi, Manyara, Njombe, Arusha na Rukwa.

Dodoma. Serikali imesema hakutakuwepo na hafla ya kitaifa na gwaride la maadhimisho ya miaka 61 ya Uhuru na badala yake Sh960 milioni fedha zilizotakiwa kutumika kwenye maadhimisho hayo zitakwenda kwenye ujenzi wa mabweni ya shule zenye uhitaji maalum.

  

Hayo yameelezwa leo Desemba 5, 2022 na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu), George Simbachawene wakati akizungumza na waandishi wa habari kuelekea maadhimisho ya miaka 61 ya Uhuru Disemba 9, 2022.


Simbachawene amesema tayari Wizara ya Nchi katika Ofisi ya Rais (Tamisemi) imebainisha Mikoa itakayonufaika na fedha hizo ambayo ni Shinyanga, Singida, Tabora, Lindi, Manyara, Njombe, Arusha na Rukwa.


Simbachawene amesema mwaka 2022 maadhimisho hayo yatafanyika katika ngazi ya wilaya kwa kufanya midahalo na makongamano ya kujadili masuala mbalimbali ya maendeleo ya kijamii.


“Kwa muktadha huu Waziri Mkuu ameniagiza kushirikiana na Waziri wa Tamisemi kufanya usimamizi, ufuatiliaji na tathmini ya midahalo na makongamano hayo ili kujiridhisha na matokeo yake,” amesema Simbachawene.


Aidha amesema kabla ya makongamano hayo, ratiba za Wakuu wa Mikoa na Wilaya zitatanguliwa na shughuli za kijamii ikiwemo kufanya usafi katika maeneo ya huduma za kijamii kama Hospitali, Shule, nyumba za wazee na nyinginezo.