Sh4.7 bilioni zawezesha vijana 1, 000 kujiajiri Mwanza

Meneja Mradi wa Vijana Maisha na Kazi kutoka Shirika la Plan International, Gadiely Kayanda akielezea mafanikio ya mradi mbele ya washiriki wa warsha ya siku moja ya kuufunga mradi huo iliyofanyika jijini Mwanza. Picha na Saada Amir

Muktasari:

Zaidi ya Sh4.7 bilioni zimewanufaisha vijana zaidi ya 1, 000 kutoka Kata 11 za Wilaya ya Nyamagana na Ilemela zinazounda jiji la Mwanza kupitia mradi wa Vijana Maisha na Kazi uliokuwa unatekelezwa na Shirika la Plan International.

Mwanza. Zaidi ya Sh4.7 bilioni zimewanufaisha vijana zaidi ya 1, 000 kutoka Kata 11 za Wilaya ya Nyamagana na Ilemela zinazounda jiji la Mwanza kupitia mradi wa Vijana Maisha na Kazi uliokuwa unatekelezwa na Shirika la Plan International.

Kupitia vikundi 58, vijana hao wamenufaika kwa kupata mafunzo ya ujasiriamali, elimu ya fedha, kilimo na ufundi huku wahitimu wakipewa vifaa vya kufanyia kazi kulingana na fani zao.

Mradi huo ulioshirikisha Shirika la kuhudumia Viwanda Vidogo nchini (Sido), Chuo cha Mafunzo na Ufundi Stadi (Veta), Tanzania Horticultural Association (Taha), Taasisi ya Social and Econimic Development Initiatives of Tanzania (Sedit) na Digital Opportunity Trust (Dot) ulioanza 2018 na kukamilika 2022.

Akizungumza leo Ijumaa, Machi 31, 2023, wakati wa warsha ya kufunga mradi huo, Ofisa mradi wa Sedit, Nahum Fungo amesema zaidi ya Sh66 milioni zimetolewa kama mikopo kwa vijana kupitia vikundi vyao.

“Vijana kutoka vikundi viwili vya watu wenye ulemavu ni miongoni mwa wanufaika kwa kupata mkopo wa zaidi ya Sh21 milioni,”amesema Fungo

Ofisa Kilimo kutoka Taha, Reymond Gervas amesema pamoja na mafunzo ya mbinu bora za kilimo, vijana waliopata fursa hiyo pia wamewezeshwa mifumo ya umwagiliaji, ushauri kuhusu kilimo cha kisasa na kuunganishwa na masoko.

Amesema licha ya changamoto kadhaa ikiwemo ya vijana wengi kutomiliki mashamba, mafunzo ya kilimo bora yamenufaisha vijana 412 na kuvuka lengo la awali la kufikia vijana 400.

Mkufunzi kutoka Sido, Maporo Maneno ameishukuru Plan International kwa kuwezesha ujenzi wa jengo lenye mashine za kusindika vyakula na kuchakata kemikali kwa gharama ya zaidi ya Sh70 milioni.

Amesema jengo na mashine hiyo siyo tu inawanufaisha vijana wote wakiwemo wasiokuwemo kwenye mradi ambao pia hupata fursa ya kutumia rasilimali hizo kutengeneza bidhaa zao.

“Vijana 157 walipata mafunzo ya usindikaji chakula, uchakataji wa kemikali, utengenezaji wa batiki, sabuni, uchomeleaji, ujasiriamali lakini pia tuliwapa ushauri. Pia tumevikopesha vikundi saba zaidi ya Sh15 milioni zilizotolewa na Plan International,”amesema Maneno

Tofauti na tatizo la marejesho linaloshuhudiwa katika vikundi vingine vya ujasiriamali, Mkufunzi huyo kutoka Sida anasema vijana wanaokopeshwa kupitia mradi huo wanarejesha vema mikopo yao.

Meneja Mradi wa Vijana Maisha na Kazi, Gadiely Kayanda amesema mradi huo umefanikiwa kufikia lengo la kuwawezesha vijana kupata mitaji, kujiajiri, kuwaunganisha na sekta binafsi pamoja na kuwajengea usawa.

“Wakati tunaanza, vijana hawakuwa na uwezo wa kujiajiri; lakini sasa wengi wao wamefungua miradi, biashara na kampuni zao. Wapo waliofungua migahawa na wengine wanafanya ujasiriamali kwa kutengeneza batiki,”amesema Kayanda

Amesema vijana hao waliopata mafunzo katika fani mbalimbali ikiwemo ufuaji vyuma, upishi, mapambo, ushonaji, useremala, ufundi mabomba na ujenzi tayari wamepewa mtaji wa vifaa kulingana fani na ujuzi wao na kukabidhiwa mikononi mwa Serikali kupitia Idara ya Maendeleo ya Jamii na maofisa vijana katika halmashauri zao kwa ajili ya usimamizi na ufuatiliaji.

Victor Herman, mmoja wa wanufaika kutoka kikundi cha Msitu ni Uhai kinachoendesha shughuli zake eneo la Luchelele Wilaya ya Nyamagana amesema mradi huo na mafunzo ya kusindika chakula, tayari kikundi chake kinamiliki mashine ya kusindika karanga yenye thamani ya zaidi ya Sh1.5 milioni yenye uwezo wa kuzalisha paketi 1, 000 kwa siku.

“Tayari tumeshazalisha faida ya Sh800, 000 tangu tuanze uzalishaji Februari, 2023. Tunatarajia kuomba mkopo kutoka halmashauri kwa ajili ya kununua mashine ya kusaga unga wa lishe,”amesema

Ofisa Maendeleo ya Jamii Mkoa wa Mwanza, Janeth Shishila amewataka vijana hao kutumia vema mafunzo na mitaji waliyopata kuongeza uzalishaji huku wakitumia mitandao ya kijamii kutangaza bidhaa zao.

Amewaagiza vijana hao kutunza na kutumia vema mashine walizopewa huku akiwaagiza maofisa Maendeleo ya Jamii na Watendaji wa Kata kufuatilia matumizi ya mashine hizo, utendaji na maendeleo ya vikundi vya vijana katika maeneo yao.