Takukuru Arusha kuanza kusikiliza kero vijiji
Arusha. Taasisi ya kuzuia na kupambana na rushwa(TAKUKURU) mkoa wa Arusha imeanzisha huduma maalum ijulikanayo kama "Takukuru inayotembea" itakayofanya kazi kila jumatano ya ya mwisho wa mwezi katika ngazi ya kata na vijiji ili kupokea kero.
Akitoa taarifa ya utendaji kazi wa taasisi hiyo kwa kipindi cha mwezi Oktoba hadi Desemba 2020 kwa waandishi wa habari Mkuu wa Takukuru mkoa wa Arusha James Ruge amesema maafisa wa tasisi hiyo watatembelea maeneo mbalimbali katika ngazi ya Kata na Vijiji kusikiliza kero za wananchi.
"Kero hizo zitafanyiwa kazi kwa mujibu wa sheria na mrejesho kutolewa kwa wahusika na kampeni hii itakuwa endelevu kwa lengo la kuwafikia wananchi katika maeneo yao na kuwasikiliza"amesema
Ruge amewaomba wananchi wote wa mkoa wa Arusha kufika katika vituo vitakavyokuwa vimepangwa kwenye maeneo yao na kutoa malalamiko yao kwa maafisa wa TAKUKURU .
"Nawahakikishia kuwa malalamiko yote yatakayopokelewa yatafanyiwa kazi kwa wakati na kupewa mrejesho"amesem
Alifafanua kuwa kuanzia October hadi Desemba 2020 taasisi hiyo imepokea taarifa 474,na kuweza kufungua majalada 212 ya taarifa hizo huku taarifa 262 kati ya taarifa hizo kuonekana kutokuangukia katika sheria ya taasisi hiyo ambapo pia wamefungua mashtaka matano mapya mahakamani huku 45 yakiendelea katika hatua mbalimbali za kimahakama.
Amesema katika kipindi hicho, mashauri 16 yametolewa uamuzi ambapo kati yake mashauri 13 jamuhuri ilishinda .