Tanzania yaruhusu usafirishaji wa wanyamapori nje ya nchi

Muktasari:

  • Serikali imeruhusu usafirishaji wa wanyamapori hai waliokuwa wamesalia kwenye mazizi na mashamba ya ufugaji baada ya zuio lililotolewa 2016.

Serikali imeruhusu usafirishaji wa wanyamapori hai waliokuwa wamesalia kwenye mazizi na mashamba ya ufugaji baada ya zuio lililotolewa 2016.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo Jumamosi Juni 4, 2022 na Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania, imesema ruhusa hiyo ni kwa kipindi cha miezi sita kuanzia Juni 6 hadi Desemba 5, 2022.

“Ili kufanikisha zoezi hili, wafanyabiashara wenye wanyamapori waliosalia kutokana na biashara ya wanyamapori hai na ambao wamefanyiwa uhakiki wanatakiwa kuwasilisha nyaraka zote muhimu katika Ofisi za Utalii na Huduma za Biashara zilizopo jijini Arusha.

“Usafirishaji wa wanyamapori hao utafanyika kupitia Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), na Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA)” imeeleza taarifa hiyo.

Taarifa hiyo imeeleza kuwa wadau watakaoruhusiwa kusafirisha wanyamapori ni wale wenye leseni ya biashara ya Nyara (TDL) zilizohuishwa kwa mujibu wa Sheria ya Uhifadhi Wanyamapori.