TARI: Zao la mhogo ni fursa kubwa kiuchumi

TARI: Zao la mhogo ni fursa kubwa kiuchumi

Songea. Wakulima wa zao la Mhogo Kanda ya Kusini wameshauriwa kuzalisha kwa wingi zao hilo lenye faida kubwa kiuchumi.

Ni kutokana na wanga wake kutengeneza taulo za kike na vidonge aina ya panado.

Wito huo umetolewa leo Ijumaa, Agosti 5, 2022 na Festo Masisila, Mtafiti  wa zao hilo kutoka Kituo cha Utafiti wa Kilimo (TARI), Naliandele wakati akizungumza na Mwananchi Digital katika ufunguzi wa maonyesho ya nanenane yaliyofanyika viwanja vya Msamala Songea, Mkoa wa Ruvuma.

Amesema zao hilo linavitu vya ziada ambapo hutumika viwandani kwa kusindika na kutengeneza vitu vingi ikiwemo keki, maandazi, biskuti na unatumika kama chakula.

“Wanga wa mhogo unatumika kubeba kidonge cha panado, wanga wa mhogo ni mzuri unauwezo mkubwa wa kunyonya majimaji na unatumika kwenye taulo za kike, pia unatumika kutengeneza alcohol ambayo ikichujwa inapatikana spirit ambayo ikipelekwa viwandani inapatikana vitakasa mikono,” amesema Masisila

Alisema wao wameshatoa elimu na kuwahamasisha wakulima kutumia mbegu bora ya mihogo na tayari wameshaandaa mashamba darasa zaidi ya 15 mkoa wa Ruvuma, Tunduru, Mbinga vijijini, Nyasa zaidi ya sita.

Aidha, ameziomba halmashauri kufanya juhudi kwa kuanzisha vikundi na  kutenga bajeti ya kununua mbegu bora ambazo zipo kwa wingi ili waweze kuwakopesha au kuzigawa bure kwa wakulima  ili wazalishe kwa wingi na wao wataweza kupata fedha kupitia ushuru ambao watawatoza.