TMDA yawakumbuka wafungwa, mahabusu mkoani Mara

Muktasari:

  •  Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA) Kanda ya Ziwa Mashariki imetoa msaada wa dawa za  kutibu binadamu za Sh23 milioni  kwa ajili ya zahanati zilizo chini ya Jeshi la Magereza Mkoa wa Mara.



Musoma. Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA) Kanda ya Ziwa Mashariki imetoa msaada wa dawa za  kutibu binadamu za Sh23 milioni  kwa ajili ya zahanati zilizo chini ya Jeshi la Magereza Mkoa wa Mara.

Msaada huo umekabidhiwa mjini Musoma leo Ijumaa  Juni 24, 2022 na meneja wa kanda hiyo, Sophia Mziray ikielezwa kuwa kuna uhitaji wa dawa kwa ajili ya kutibu wafungwa na mahabusu.

Akizungumza wakati wa kukabidhi msaada huo, meneja huyo amesema  ofisi yake ilibaini  uhitaji ya dawa baada ya kufanya ziara katika mkoa wa Mara kwa jili ya kampeni ya kutokomeza matumizi ya bidhaa za tumbaku mkoani humo.

"Dawa hizi ni kwa ajili ya kutibu magonjwa mbalimbali ya binadamu na tunaamini  zitasaidia  kupunguza upungufu wa dawa kwenye zahanati za Magereza hivyo kuoboresha huduma zitolewazo kwa wafungwa na mahabusu pamoja na watumiaji wengine" amesema

Mganga mkuu wa mkoa wa Mara, Dk Juma Mfanga ameutaka uongozi wa Magereza kuhakikisha dawa hizo zinatumika kama ilivyokusudiwa huku akiahidi kuendelea kuwasiliana na TMDA  ili kuleta msaada wa aina hiyo kadri itakavyowezekana.

" Kawwida dawa za serikali zinakuwa na nembo maalum  lakini kwa hapa najua TMDA  hawajaweka nembo, sasa hali hiyo isitumike kama kigezo cha dawa hizi  kupelekwa kwingine ikiwepo kwenye  maduka kwa ajili ya kuuzwa isipokuwa ni kwa ajili ya matumizi ya magereza kama ilivyokusudiwa," amesema

Mkuu wa Magereza Mkoa wa Mara,  Hospitius Mendi mbali na  kushukuru kwa msaada huo ameiomba taasisi hiyo kuendelea kutoa msaada wa aina hiyo kwani mahitaji ya dawa ni makubwa tofauti na hali halisi ingawa hakutoa takwimu.

Amesema dawa hizo zitapelekwa kwenye zahanati sita za  magereza zilizopo mkoani Mara na kuahidi kuwa zitatumika kwa matumizi yaliyokusudiwa.

" Serikali huwa inaleta dawa kwa zahanati zetu kama kawaida lakini kama mnavyojua mahitaji yapo kila siku hivyo ushiriki wa waduu wengine ni muhimu ili kuboresha zaidi huduma zetu kwa ustawi wa jamii yetu," amesema Mendi.