Ujumbe kamati za Bunge kwa reli ya Tazara
Muktasari:
- Kamati za Miundombinu na Bajeti zaitaka Tazara kukamilisha majadiliano ili ujenzi wa reli hiyo uanze mara moja ili kuchochea maendeleo kwa mataifa ya Tanzania, Zambia na ukanda wote.
Dar es Salaam. Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu na Kamati ya Bajeti zimeutaka uongozi wa Reli ya Tanzania Zambia (Tazara) kuongeza kasi katika kukamilisha majadiliano ili reli hiyo ianze kukarabatiwa.
Hayo yanaelezwa huku tayari mchakato wa kuikarabati reli hiyo unaendelea baada ya China, Tanzania na Zambia kutia saini ya makubaliano ya awali yanayolenga kuboresha usafirishaji kwenye ukanda huo.
Mwenyekiti wa Kamati ya Miundombinu, Seleman Kakoso Jijini Dar es Salaam leo,11 Novemba, 2024 wakati wa ziara ya kamati hizo zilizotembela ofisi za makao makuu.
Kakoso amesema kwa nia nzuri ya Rais Samia Suluhu Hassan na Rais wa Zambia Dk Hakainde Hichilema kwa kushirikiana na mshirika wao Nchi ya China wameamua kuifufua reli ya Tazara na mkataba umeshasainiwa.
"Kwa nia hii nzuri iliyooneshwa kamati inaitaka Tazara ifanye haraka katika kukamilisha majadiliano ya kukamilisha mifumo ya kuanza ukarabati wa reli sambamba na vitendea kazi, mabehewa na vichwa vya treni" amesema Kakoso
Amesema reli hiyo ni ya nchi mbili hivyo kwa serikali ya Zambia kupitisha mzigo kwa asilimia 30 pekee kwenye reli hiyo inatengeneza mgawanyo na inakuwa hujuma na kutoa rai mzigo kutoka Zambia uongezeke mpaka asilimia 50 ili kuiimarisha reli hii
Kakosa ameutaka uongozi wa taasisi hiyo ufikirie kuongeza bajeti yake kutoka Dola 36 bilioni kwa nchi zote mbili kwani ilivyo sasa ni kidogo ili reli isimame inatakiwa kuongezewa mtaji.
“Uongozi unatakiwa kuwa na ubunifu na kufanya kazi kwa uzalendo ili kuiimarisha reli kibiashara. Reli hii inahitaji ubunifu mkubwa kwa waliopewa dhamana ili iweze kujiendesha na kusimama yenyewe bila utegemezi maana fursa za mzigo zipo," amesema Kakoso
Mwenyekiti wa kamati ya bajeti, Oran Njeza amesema pamoja na changamoto zote za Tazara inabidi wafikirie kubadili muundo wa uendeshaji.
Amesema Tazara ni ya nchi mbili ila kutokana na muudo wake wa uendeshaji wa mwaka 1968 inakuwa kama haina mwenyewe hivyo badala ya kuangalia biashara wanaangalia jinsi ya kugawana nafasi hali ambayo inaidhoofisha.
“Serikali inatakiwa kuangalia ni namna gani ianze mpango wa mda mfupi wa kuifanya Tazara kuwa shirika na kuhakikisha kunakuwa na mkakati wa pamoja na Bandari na Reli ya Kisasa ya SGR.
Wenyeviti wa kamati zote wametoa rai kwa wabunge wa serikali ya Zambia wanaohusika na miudombinu kukutana na wabunge wa Tanzania ili kuwa na uelewa wa pamoja wa jinsi ya kuliendesha shirika kwa maslah ya pande zote.
Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Ludovick Nduhiye amesema Wizara imepokea maoni na michango yote ya kamati zote mbili yenye lengo la kuibadilisha na kuiimarisha reli hiyo mengi ni maelekezo yatafanyiwa kazi vizuri.
Awali Mkurugenzi mtendaji wa Tazara, Bruno Ching'andu amesema Tazara ni mamlaka ya pamoja kati ya Serikali ya Tanzania na Zambia iliyoanzishwa mwaka 1975.
Amesema lengo kuu la Tazara ni kuendesha huduma za reli kati ya bandari ya Dar es salaam mpaka Zambia na inachukua jukumu muhimu katika usafirishaji wa abiria na mizigo pia katika uimarishaji wa mahusiano ya kiuchumi na kibiashara baina ya nchi hizo.
“Pamoja na changamoto mbalimbali za uendeshaji wa reli ya Tazara kwa kushirikiana na watumiaji binafsi mapato yameongezeka japo chini ya kiwango cha kutopata hasara,”amesema.