Uwekezaji katika hatua za awali za ukuaji wa mtoto unalipa
Muktasari:
Hakuna kitu kinachoizidi furaha ya kuwa na mtoto kwa wazazi, lakini je, furaha ya wazazi hao bado itadumu wakimuona mtoto wao amedumaa kwa kutokunyonyeshwa vizuri katika hatua za awali za ukuaji wake?
Na Stella Kimambo
Hakuna kitu kinachoizidi furaha ya kuwa na mtoto kwa wazazi, lakini je, furaha ya wazazi hao bado itadumu wakimuona mtoto wao amedumaa kwa kutokunyonyeshwa vizuri katika hatua za awali za ukuaji wake?
Tanzania, ikiwa ni nchi ya uchumi wa kati, inahitaji nguvukazi imara, lakini lengo hilo haliwezi kufikiwa kwa sababu maelfu ya watoto hawakunyonyeshwa maziwa ya mama au kupatiwa madini muhimu ndani ya kipindi cha siku 1,000 (tangu kutungwa mimba hadi miaka miwili), hivyo kusababisha kuwa na kizazi cha nguvukazi yenye udumavu.
Kudumaa, kutokuwa na uwezo wa kufikia urefu unaohitajika kwa umri maalum, huathiri asilimia 31.8 ya watoto walio chini ya umri wa miezi 59. Watoto waliodumaa huwa na athari za kudumu ambazo hugusa vizazi kwa vizazi.
Lishe ndiyo siri iiliyopo nyuma ya ukuaji wa mapema wa mtoto. Ubongo hukua haraka katika siku 1,000 za kwanza za mtoto kuliko wakati mwingine wowote katika maisha ya mtu. Na, ili kuchochea ukuaji wa haraka wa mtoto, ubongo unahitaji kiasi sahihi cha virutubisho kwa wakati unaofaa.
Kupitia mpango wa AGRI-CONNECT unaofadhiliwa na Umoja wa Ulaya, Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO), Serikali na Umoja wa Ulaya (EU) walizindua kampeni ya LISHE BORA NI MTAJI (Lishe Bora ni Uwekezaji) Kitaifa kwa Tanzania Bara na Zanzibar, kuhamasisha ulaji bora unaozingatia vyakula vinavyopatikana nchini.
Kampeni hiyo inatarajiwa kuwafikia watu milioni 32 kupitia programu za mapishi, ziara za elimu ya lishe kwa daladala (basi dogo), mafunzo kwa vijana wa kike, na uanzishwaji wa maeneo ya vyakula vya asili (msosi asilia), kwa kutumia mitandao ya kitamaduni na kijamii.
Tofauti na uwekezaji mwingine wa maendeleo, kuwekeza katika hatua za awali za ukuaji wa mtoto hutoa thamani bora zaidi ya pesa ikilinganishwa na matatizo ambayo mtoto anaweza kukabiliana nayo baadaye maishani.
Timiza wajibu wako na uwekeze katika ukuaji wa mapema wa watoto wako!
*Mtaalamu wa Usalama wa Chakula na Lishe, FAO Tanzania