Wachache wajitokeza kupiga kura Konde

Muktasari:

  •  Wakati uchaguzi wa marudio Jimbo la Konde ukifanyika, imeonekana kuwepo idadi ndogo ya Wananchi katika vituo vya kupigia kura.


Pemba. Wakati uchaguzi wa marudio Jimbo la Konde ukifanyika, imeonekana kuwepo idadi ndogo ya wananchi katika vituo vya kupigia kura.

Uchaguzi huo unafanyika leo Jumamosi Oktoba 9, 2021 ikiwa ni wa marudio baada ya ule wa awali uliofanyika Julai 18 aliyetangazwa kushinda, Sheha Mpemba Faki (CCM) kujiuzulu kabla ya kuapishwa.

Mwananchi digital imeshuhudia idadi ndogo ya wananchi wanaojitokeza katika vituo hivyo huku wengi kati yao wakiwa wanawake.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti na Mwananchi digital baadhi ya wananchi hao wamesema shughuli hiyo inaendelea vizuri kwa amani na utulivu.

"Nimemaliza kupiga kura, sijapata shida yoyote, kuna utulivu na amani ipo," amesema Sada Ali Juma

Khadija Talib amesema "mwanzoni niliangalia jina langu nikalikosa lakini baadaye nimeruhusiwa kupiga kura baada ya kuliona jina langu.

Naye Msimamizi wa uchaguzi wa Jimbo hilo,  Abdalla Said Hamad amesema uchaguzi huo unaendelea vizuri na hawajakumbana na changamoto.

Kuhusu idadi ndogo ya Wananchi wanaojitokeza, Hamad amesema "watu sio wachache kiasi hicho bali wanafika na kupiga kura kisha wanaondoka.