Wahamiaji haramu 40 wakamatwa Iringa

Muktasari:

Jeshi la Polisi mkoani Iringa linawashikilia watu 40 wanaodaiwa kuwa raia wa Ethiopia kwa tuhuma za kuingia nchini bila kibali kupitia mpaka wa Namanga wakisafirishwa kuelekea mpaka wa Tunduma mkoani Songwe.

Iringa.Jeshi la Polisi mkoani Iringa linawashikilia watu 40 wanaodaiwa kuwa raia wa Ethiopia kwa tuhuma za kuingia nchini bila kibali kupitia mpaka wa Namanga wakisafirishwa kuelekea mpaka wa Tunduma mkoani Songwe.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Alhamisi Januari 13, 2022 Kamanda wa Polisi Mkoa wa Iringa, Allan Bukumbi amesema raia hao walikamatwa jana maeneo ya Ugwachanya kata ya Mseke Manispaa ya Iringa.

Kamanda Bukumbi amesema kuwa askari polisi wakiwa kwenye doria walifanikiwa kukamata gari aina ya fuso likiwa limetelekezwa barabara kuu ya Iringa-Mbeya na dereva ambaye hajajulikana.

“Upekuzi ulifanyika ndani ya gari hilo na kukuta wahamiaji haramu 40 wote raia wa Nchini Ethiopia wakiwa wameingia nchini bila kibali ambapo watuhumiwa hao watafikishwa mahakamani mara baada ya upelelezo kukamilika”amesema Bukumbi