Wamwaga chakula msibani, wadai marehemu hakuwa akipewa chakula alipokuwa hai

Wamwaga chakula msibani, wadai marehemu hakuwa akipewa chakula alipokuwa hai

Muktasari:

  • Waendesha bodaboda wa kituo cha Kisangiro kata ya Kilema Kaskazini wilayani Moshi Mkoa wa Kilimanjaro wamevamia msiba wa Lenard Abel (20) na kumwaga chakula na pombe kwa madai kuwa marehemu alikuwa hapewi chakula alipokuwa hai.

Moshi. Waendesha bodaboda wa kituo cha Kisangiro kata ya Kilema Kaskazini wilayani Moshi Mkoa wa Kilimanjaro wamevamia msiba wa Lenard Abel (20) na kumwaga chakula na pombe kwa madai kuwa marehemu alikuwa hapewi chakula alipokuwa hai.

Walifika katika msiba huo saa 9 alasiri jana Jumatatu Mei 3, 2021 baada ya mazishi wakati mwenyekiti wa ukoo akitoa ratiba ya chakula na kumwaga chakula hicho kitendo kilichozua tafrani na waombolezaji kulazimika kutimua mbio.

Shuhuda wa tukio hilo, Lucy Lyimo amesema kundi hilo la vijana lilifika msibani na kuvamia jikoni na kuanza kumwaga chakula na pombe aina ya mbege sambamba na kuvunja viti.

“Wakati mwenyekiti wa ukoo akitoa ratiba ya chakula kulitokea kundi la vijana zaidi ya ishirini wakipiga ukunga na kusema huyu marehemu kipindi akiwa hai alikuwa hapewi chakula iweje leo amekufa chakula kipo na pombe, " amesema Lucy akibainisha wakati wakisema hayo walikuwa wakielekea ilipohifadhiwa pombe na chakula

Amesema walipomwaga chakula na pombe waliwasha mishumaa na kuelekea makaburi yalikofanyika mazishi.

Mwenyekiti wa kijiji cha Kyou, Paul Lyimo amesema wakati vijana wakifanya vurugu za kumwaga chakula na vinywaji Padri wa Parokia ya Kilema aliyeendesha ibada ya mazishi aliwafuata kuwaomba wasifanye vurugu ila hawakusikia.

"Padri aliwapigia hadi magoti kuwaomba wasifanye hivyo lakini waliendelea kumwaga chakula huku wakipiga ukunga na baada ya hapo walienda kuwasha mishumaa kwenye kaburi na kutawanyika," amesema.