Wanafunzi waaswa kujiepusha na matumizi mabaya ya mitandao

Wanafunzi waaswa kujiepusha na matumizi mabaya ya mitandao

Muktasari:

  • Wanafunzi wameaswa kujiepusha na matumizi mabaya ya mitandao hasa katika kipindi hiki cha mapinduzi ya sayansi na teknolojia, ambacho matumizi ya mitandao haiepukiki.

Dar es Salaam. Wanafunzi wameaswa kujiepusha na matumizi mabaya ya mitandao hasa katika kipindi hiki cha mapinduzi ya sayansi na teknolojia, ambacho matumizi ya mitandao haiepukiki.

Vilevile wazazi wametakiwa kuhakikisha wanafuatilia kwa ukaribu matumizi ya mitandao kwa watoto wao, kwani matumizi yake yasiosahihi yanachangia kwa asilimia kubwa mmomonyoko wa maadili katika jamii.

Hayo yamesemwa leo Oktoba 14 na mgeni rasmi, Jessica Kikumbi ambaye ni mkurugenzi wa Kitambaa Cheupe Microfinance, katika mahafali ya 16 ya kidoto cha nne yaliyofanyika katika shule ya sekondari Magoza iliyopo Tabata jijini hapa.

“Matumizi mabaya ya mitandao ni mdudu mkubwa katika mmomonyoko wa maadili ni mitandao ya kijamii,” amesema.

Vilevile amewapongeza wanafunzi wa kidato cha nne kwa hatua ya kimasomo waliofikia mbali na changamoto za Uviko-19 na kuwaasa wanafunzi hao kutoridhika na ngazi ya elimu waliofikia.

“Elimu ya kidato cha nne mliofikia ni mlango tu wa kufikia maendeleo makubwa zaidi katika masomo yenu na sio mwisho wa kuendelea kuitafuta elimu,”amesema.

Naye Mwalimu mkuu washule hiyo, Kalunde Sigera mbali na kumshukuru mgeni rasmi pia alitumia fursa hiyo kuishukuru serikali kwa kuanzisha utoaji wa elimu bure kwani imeongeza wanafunzi shuleni.

“Mbali na hilo pia kupitia fedha zilizotengwa kwa ajili ya ujenzi wa madarasa na uboreshaji wa miundombinu shule itawezeshwa kujengewa vyoo na chumba cha komputa,” amesema.

Kwa upande wake ofisa Elimu Kata ya kisukulu, Gerald Boniface amewata wanafunzi kujitahidi kuwa na nidhamu katika kila wanachokifanya kawani ndiyo msingi wa kila kitu katika maisha.

“Elimu inaenda sambamba kabisa na nidhamu hivyo wanafunzi kama mnataka kufikia malengo yenu mnapaswa kuwa na nidhamu katika kila kitu mnachofanya,” amesema.