Wananchi wajitokeza kupiga kura, amani yatawala Jimbo la Konde

Wananchi wajitokeza kupiga kura, amani yatawala Jimbo la Konde

Muktasari:

  • Wananchi wachache wanaonekana kujitokeza katika uchaguzi mdogo wa  Jimbo la Konde.

Unguja. Wananchi wachache wanaonekana kujitokeza katika uchaguzi mdogo wa  Jimbo la Konde.

Uchaguzi huo unafanyika  leo Jumapili Julai 18, 2021 kutokana na kifo cha aliyekuwa mbunge wa Jimbo hilo Khatib Said.

Wakizungumza na Mwananchi baadhi ya wapiga kura hao wamesema hali ni shwari na wamepata haki yao ya kikatiba kuchagua mgombea wanayemtaka.

"Mimi nimeshapiga kura hali ni shwari hakuna tatizo lolote tunamshukuru Ala tuendelee mpaka mwisho," amesema Tatu Hamza.

Mwanahamisi Mwinyimvua amesema mwanzoni alipata changamoto ya kukataliwa kupiga kura kwasababu ya kutoonekana jina lake kwenye daftari la mpigakura.

"Nilishangaa jina langu pale ukutani lipo, kitambulisho ninacho lakini nilipoingia ndani naambiwa hawaoni jina langu," amesema.

Akizungumzia changamoto hiyo msimamizi wa uchanguzi wa jimbo hilo, Yassin Khamis amesema "Ni kweli ilijitokeza hiyo shida ya kutoonekana baadhi ya majina lakini nimelishghulikia jambo hilo ilikuwa ni suala la uelewa tu."

Naye Mwakilishi wa Jimbo la Konde, Zawadi Ali Khamis amesema kuna utulivu wa kutosha na hawajaona changamoto yoyote.

Kuhusu suala la uchahe wa waliojitokeza kupiga kura amesema "Tunajua kasumba ya wananchi huwa wanasubiri muda uende waje ila wengine wanaanza kufanya shughuli zao ila tunaamini wataongezeka kadri muda unavyoenda.